Kazeni sheria za barabarani kuzuia ajali, Wetang’ula aambia Wabunge
Spika wa Bunge la Kitaifa Moses Wetang’ula amewaomba Wabunge kuweka mkazo zaidi katika sheria zinazodhibiti sekta ya uchukuzi nchini.
Spika Wetang’ula alionyesha wasiwasi wake kuhusu kuongezeka kwa ajali za barabarani, akibainisha kwamba taifa linapoteza maisha kwa wingi kutokana na ajali za barabara. Alisisitiza umuhimu wa taifa kutafakari kwa kina jinsi ya kupunguza tatizo hili.
“Tunakemea ukosefu wa uwajibikaji wa dereva wa lori aliyehusika na ajali mbaya katika makutano ya Malaha ambayo ilisababisha vifo vya watu 15. Inasikitisha kwamba zaidi ya watu 21 wamefikishwa katika hospitali mbalimbali, huku wawili wakiwa wanahitaji matibabu maalumu kwa dharura,” alisema Spika Wetang’ula.
Spika Wetang’ula, ambaye alitembelea waathiriwa hospitalini aliitaka NTSA kuchukua hatua haraka kuhakikisha madereva wasio makini wanaondolewa barabarani.
“Naomba Mahakama zetu zizingatie kinachotokea katika jamii yetu. Ikiwa hufai kuwa barabarani, basi kaa mbali. Ikiwa uko barabarani na hufuatilii sheria, basi unastahili adhabu,” aliongeza.
Spika Wetang’ula alisema Rais William Ruto ameahidi serikali itasaidia familia zilizoathirika na wagonjwa walioko hospitali. Alibainisha kuwa Serikali ya Kaunti itagharamia bili za matibabu ya wote waliopata madhara.
Spika pia alitangaza kuundwa kwa kamati ya mazishi inayoongozwa na Mbunge wa Webuye East Marthin Wanyonyi Pepela na Mwakilishi wa Wanawake Bungoma Catherine Wambilianga kupanga mazishi ya waliofariki.
Mmoja wa wakazi walioathirika, Isaac, ambaye alipoteza mkewe, alisema ana matumaini kwamba familia yake ya watu watatu, wakiwemo baba yake na kaka yake waliovunjika mifupa, watapona na kuruhusiwa kutoka hospitali.
Daktari Mkuu wa Hospitali ya Rufaa ya Kaunti ya Webuye, David Wanikina, alisema wagonjwa wawili wa kiume watahitaji matibabu maalumu.