Kero ya bodaboda yalemaza usafiri jijini matatu zikigoma zikilalamikia utovu wa nidhamu
SERIKALI imemulikwa kwa kufeli kudhibiti utovu wa nidhamu unaozidi kukithiri katika sekta ya bodaboda, kero ambalo mara kwa mara limehatarisha maisha na kutatiza uchukuzi wa umma.
Sekta ya bodaboda inayoajiri zaidi ya Wakenya milioni na kuzalisha mabilioni katika mapato ya kila mwaka, imezidi kukiuka sheria ikijasirishwa na ushawishi wa kisiasa na historia ya serikali kutochukua hatua.
Licha ya maonyo ya awali na majaribio ya kuanzisha sheria kali, serikali mara kwa mara imenywea kutokana na shinikizo, na kuruhusu waendeshaji bodaboda wahalifu kutekeleza ‘haki’ bila hofu wala kuadhibiwa.
Shambulizi na uteketezaji wa magari hivi majuzi ulisababisha mgomo wa waendeshaji matatu chini ya Muungano wa Wamiliki Matatu (MOA) na kuwaacha abiria wakiwa wamekwama kote katika jiji kuu, Nairobi jana.
Magari yanayotumia mikondo mikuu kama vile barabara kuu za Thika, Ngong, Mombasa na Jogoo yaliwaacha abiria na kuwalazimu wengi kutembea masafa marefu au kuwalipa wahudumu wa bodaboda kiwango cha juu cha nauli kuliko kawaida.
Mnamo Januari 23, 2026, wahudumu wa bodaboda waliteketeza basi la kampuni ya Forward Travellers baada ya ajali ambapo basi hilo lilidaiwa kumgonga mwendeshaji pikipiki.
Shambulizi hilo ni sawa na visa vinginevyo mwaka jana vilivyohusu mabasi ya kampuni za Super Metro na City Shuttle na limezua upya wasiwasi kuhusu ukiukaji sheria wa sekta hii.
Mwaka uliopita, Seneta Boni Khalwale (Kakamega) alilazimika kuondoa Mswada kuhusu Usafiri wa Umma (Kudhibiti Pikipiki) 2023 kufuatia malalamishi kutoka kwa wahudumu.
Mswada huo ulikusudiwa kudhibiti ukosefu wa nidhamu ikiwemo kuendesha pikipiki kinyume cha sheria za trafiki, kutumia vijisehemu vya wapitanjia na kukosa kuvaa kofia au koti za rangi za kuangaza.
Aidha, ulipendekeza faini kali kwa waendeshaji pikipiki wanaokusanyika kuwatishia au kuwadhuru wengine kufuatia ajali, ikiwemo faini ya hasi Sh100,000 au kifungo cha jela kwa hadi mwaka mmoja.
“Mwendeshaji pikipiki yeyote anayeungana na wengine kutia hofu, kutishia au kudhuru mtu mwingine, ikiwemo wakati wa ajali, ana hatia,” mswada ulisema.
Japo Seneti ilipitisha pendekezo hilo la sheria, Dkt Khalwale aliliondoa kabla ya kujadiliwa kwenye Bunge la Kitaifa, kuashiria ushawishi wa sekta hiyo kisiasa.
Licha ya ahadi alizotoa awali aliyekuwa waziri wa usalama wa ndani, Fred Matiang’i, mnamo 2022, kuwazima waendeshaji pikipiki wahuni, hakuna hatua yoyote thabiti imetekelezwa.
Miaka minne baadaye, wanabodaboda wanazidi kuwa jasiri kufanya wanachochukulia kuwa “haki” kila wakati mmoja wao anapohusika kwenye ajali.