Kindiki abadili mbinu, apunguza mashambulizi dhidi ya wapinzani Mlimani
NAIBU wa Rais Kithure Kindiki ameanza kubadili mkakati wa kisiasa katika eneo la Mlima Kenya, akionekana kupunguza mashambulizi dhidi ya wapinzani na badala yake kusisitiza umoja na maendeleo huku vita vya kisiasa kuelekea uchaguzi wa 2027 vikizidi kushika kasi.
Prof Kindiki anaonekana kuachana na msimamo mkali aliokuwa nao awali dhidi ya hasimu wake mkuu Rigathi Gachagua, kiongozi wa DCP, na sasa anasisitiza umoja wa jamii na ajenda ya maendeleo kama njia ya kuimarisha nafasi ya serikali ya muungano wa Kenya Kwanza.
Mabadiliko hayo yanaonekana kupitia mikutano ya kisiasa iliyopangwa kwa umakinifu, ishara kwamba muungano unaoongozwa na Rais William Ruto umegundua kuwa siasa za Mlima Kenya zinabadilika kwa kasi huku makundi pinzani yakijipanga upya.
Katika hotuba zake kwenye mikutano ya hadhara Embu na Tigania Magharibi, Kaunti ya Meru, Kindiki alichukua msimamo wa upatanisho, akiepuka mashambulizi ya moja kwa moja hata anapokosolewa.
“Mimi ni kiongozi na kuna leo na kesho. Hata baada ya uongozi tutabaki jamii moja. Sina shida na kiongozi yeyote, hata wanaonitusi. Nimewasamehe bila masharti,” alisema.
Kauli hiyo ilifasiriwa kama ujumbe wa moja kwa moja kwa Gachagua, huku wachambuzi wakisema ni ishara ya mkakati mpya unaolenga kupunguza migawanyiko ya kisiasa katika eneo hilo.
Kulingana na mchambuzi wa siasa Prof Gitile Naituli, hatua hiyo ni ya kimkakati.
“Kindiki anatambua hali halisi mashinani ambapo Gachagua anaonekana kupata uungwaji mkubwa, hivyo anajaribu kujenga nafasi ya kisiasa,” alisema.
Hata hivyo, anaonya kuwa mabadiliko hayo huenda yasitoshe kubadili mitazamo ya wapigakura ambao tayari wanaonekana kuwa na misimamo thabiti.
Mkakati wa Kindiki unajikita katika mikutano ya mara kwa mara katika makazi yake ya Irunduni, Kaunti ya Tharaka Nithi, ambapo anakutana na viongozi wa mashinani, wataalamu, vijana na viongozi wa dini ili kujenga mtandao wa kisiasa.
Mikutano hiyo inalenga kuimarisha nafasi ya Rais Ruto katika uchaguzi wa 2027, kujadili mustakabali wa kisiasa wa Mlima Kenya na kukabiliana na ushawishi wa makundi yanayomuunga mkono Gachagua na aliyekuwa Rais Uhuru Kenyatta.
Katika mikutano hiyo, Kindiki amekuwa akisisitiza kuwa kumuunga Ruto mwaka wa 2027 ni njia ya haraka kwa eneo hilo kupata urais mwaka wa 2032.
“Hatutakuwa na chaguo ila kumchagua tena Rais Ruto. Baada ya hapo tutasubiri miaka mitano tu, ndipo 2032 tufikie lengo letu,” alisema.
Hoja hiyo inalenga kuwashawishi wakazi wa Mlima Kenya kuwa ni bora kusubiri muda mfupi kuliko kuchelewesha ndoto ya urais kwa muda mrefu.
Hata hivyo, wakosoaji wanasema ujumbe huo unapoteza mvuto huku baadhi ya wakazi wakionyesha kutamaushwa na serikali ya sasa.
Gachagua, kwa upande wake, amehoji nia ya serikali, akitaja masuala ya maandamano ya vijana, madai ya ufisadi na kile anachodai ni juhudi za kugawanya eneo hilo.
Mbali na siasa, Kindiki ameongeza uwepo wake mashinani kwa kuzindua miradi ya maendeleo katika eneo la Mlima Kenya Mashariki ili kuimarisha ufuasi.
Miongoni mwa miradi hiyo ni daraja la Nithi, ambalo amesema litakuwa mojawapo ya madaraja makubwa nchini likikamilika, pamoja na barabara, masoko, miradi ya maji na miundomsingi ya elimu.
Tume ya Uchaguzi (IEBC) inakadiria kuwa zaidi ya wapigakura milioni 1.7 watakuwa katika kaunti za Meru, Embu na Tharaka Nithi ifikapo 2027, jambo linalofanya eneo hilo kuwa muhimu kisiasa.
Wachambuzi wanasema mkazo wa Kindiki katika Mlima Kenya Mashariki ni juhudi za kuimarisha ngome yake ili kufidia kupotea kwa umaarufu katika maeneo mengine.
Aidha, anajaribu kusawazisha maslahi ndani ya muungano wa serikali, hasa ODM ikiongeza ushawishi wake na hata kutaka ipewe kiti cha unaibu wa rais.
Hata hivyo, mazingira ya kisiasa katika eneo la Mlima Kenya yanaendelea kubadilika kwa kasi, hasa kutokana na ushirikiano unaochipuka kati ya Uhuru Kenyatta na Gachagua, ambao unaweza kuathiri pakubwa siasa za kitaifa.
Kwa sasa, mkakati wa Prof Kindiki wa maridhiano, maendeleo na ahadi za kisiasa za muda mrefu unaonekana kuwa jaribio la kuimarisha uungwaji katika eneo hilo.
Lakini huku muda ukizidi kuyoyoma, haijulikani iwapo mbinu hiyo itatosha kukabiliana na ushindani mkali wa kisiasa unaoendelea kujitokeza.