Kindiki kona mbaya tishio kutoka pande tatu zikimuandama
NAIBU wa Rais Prof Kithure Kindiki anakabiliwa na mtihani mkubwa wa kisiasa huku mjadala kuhusu iwapo atasalia mgombeaji mwenza wa Rais William Ruto katika Uchaguzi Mkuu wa 2027 ukizidi kushika kasi na kuzua maoni mseto.
Japo amehudumu kwa chini ya miaka miwili tangu achukue nafasi hiyo, Prof Kindiki sasa ana kibarua cha kupambana na changamoto kutoka pande tatu zinazotishia mustakabali wake kisiasa.
Mtihani wa kwanza unatokana na aliyekuwa Naibu wa Rais Rigathi Gachagua, ambaye ameanzisha kampeni kali katika ukanda wa Mlima Kenya Mashariki, ngome ya kisiasa ya Profesa Kindiki.
Baada ya ushindi wa chama chake katika uchaguzi mdogo wa Ol Kalou, Bw Gachagua ameahidi kufuatilia kila ziara ya Rais Ruto katika eneo hilo kwa mikutano ya kisiasa akinuia kupunguza ushawishi wa serikali kabla ya uchaguzi wa mwaka ujao.
Tangu ateuliwe naibu rais (DP), Prof Kindiki amekuwa akiongoza hafla za kufungua miradi ya maendeleo katika eneo hilo ikiwemo uzinduzi wa barabara, nyumba za gharama nafuu na hata miradi ya kilimo.
Baadhi ya wafuasi wake wanasema ziara hizo zimedumisha imani ya wakazi kwamba eneo la Mlima Kenya bado lina sauti serikalini, ila Bw Gachagua anataka kuhakikisha imani hiyo haigeuki kuwa kura kwa Kenya Kwanza 2027.
Kibarua cha pili kinatokana na siasa ambazo zinaendelea ndani ya Kenya Kwanza baada ya ushirikiano mpya na ODM.
Hii ni kwa sababu viongozi wa ODM wameweka wazi kuwa wanataka nafasi ya naibu rais ikiwa ushirikiano wao na UDA utaendelea kabla na baada ya uchaguzi wa 2027.
Baadhi ya viongozi wa chama hicho, akiwemo Naibu Kiongozi Simba Arati na Kiongozi wa Wachache katika Bunge la Kitaifa Junet Mohamed, wamesema nafasi hiyo inapaswa kutolewa kwa ODM.
Chama hicho kimewataja Gavana wa Homa Bay Gladys Wanga, Waziri wa Madini Hassan Joho na Wycliffe Oparanya kama wanaotosha kuwa mgombeaji mwenza wa Rais Ruto.
Wadadisi wa masuala ya kisiasa wanasema msukumo wa ODM unamweka Profesa Kindiki katika hali ngumu kwa sababu Rais Ruto anaweza kulazimika kutathmini kusalia naye au kumwondoa na kutumia nafasi hiyo kuimarisha ushirikiano na ODM.
Prof Kindiki amejipata katika hali ngumu zaidi baada ya taarifa kudai kuwa baadhi ya majukumu yaliyokuwa yakihusishwa na afisi ya naibu rais yamehamishiwa kwa Kinara wa Mawaziri Musalia Mudavadi.
Hata hivyo, Prof Kindiki amekanusha madai hayo na kuyataja kuwa habari za uongo.
Mkuu wa Uchumi wa Ubunifu na Miradi Maalum katika Afisi ya Rais Dennis Itumbi naye alisisitiza kuwa majukumu ya kila afisi yamebainishwa kwenye Katiba na sheria, na hakuna mamlaka yaliyoondolewa kutoka kwa Naibu Rais.
Licha ya magumu yanayomkabili Profesa Kindiki, wadadisi kadhaa wa kisiasa wanaamini bado ndiye chaguo bora zaidi kwa Rais Ruto.
Wanasema ameonyesha uaminifu, utulivu, uwezo na amekuwa akiepuka migogoro ya hadharani na rais, tofauti na waliomtangulia.
Mdadisi wa masuala ya kisiasa Steve Ngari anasema Profesa Kindiki ameonyesha sifa zinazotarajiwa kwa afisi yake na anafaa kuendelea kusalia katika kambi ya Rais.
Aidha, kura za maoni za Infotrak zimemweka Prof Kindiki kileleni mwa wanaopendelewa kuwa mgombea mwenza wa Rais Ruto kwa asilimia 34, akifuatiwa na Gladys Wanga kwa asilimia 11 na Oburu Oginga kwa asilimia tano.
Kwa mujibu wa Bw Ngari, kumwondoa Prof Kindiki kunaweza kuwakera wapigakura wa Mlima Kenya Mashariki ambao wanaona nafasi ya naibu rais kama ishara ya ushawishi wao serikalini.
“Kazi ya Naibu Rais ni kuhudumu kama msaidizi wa karibu wa Rais. Kindiki ameonyesha sifa ambazo zinamwezesha kuendelea kuhudumu kwa wadhifa,” akasema Bw Ngari.
Pia, kunaweza kuibua taswira kwamba uaminifu na utendakazi hauthaminiwi ndani ya Kenya Kwanza.
Waziri wa Utumishi wa Umma Geoffrey Ruku naye ameendelea kumtetea Prof Kindiki, akisisitiza kuwa hakuna nafasi iliyo wazi ya naibu rais na kwamba, Rais Ruto tayari ameamua mgombea wake mwenza.