Kiongozi mkuu wa Iran Ayatollah Khamenei auawa kwenye shambulio la Israel-Amerika
KIONGOZI Mkuu wa Iran Ayatollah Ali Khamenei ameuawa kwenye shambulio lililotekelezwa kwa ushirikiano wa Israel na Amerika, vyanzo katika serikali ya Israel vimeambia mashirika makuu ya habari.
Kulingana na vyanzo hivyo ambavyo vilizungumza na shirika la habari la kimataifa la Reuters na CNN, Mkuu huyo ambaye pia ndiye kiongozi wa kidini aliuawa wakati uvamizi ulipofanywa ukimlenga yeye binafsi na Rais Masoud Pezeshkian.
Hatima ya Rais Pezeshkian bado haijatambulika kufikia wakati wa kuandika taarifa hii.
Awali, Waziri Mkuu wa Israel Benjamin Netanyahu alikuwa amedokeza uwezekano wa Ayatollah kuwa alifariki, pale aliposema “kuna dalili nyingi kwamba hayupo nasi” bila kueleza wazi wazi iwapo mkuu huyo aliuawa au la.
Khamenei aliongoza taifa hilo na kuongeza uwezo wa kijeshi ikiwemo kuwa na juhudi za kujipatia zana za kinyuklia, jambo lililokera pakubwa Amerika na washirika wake na kuitaja Iran kuwa adui wake nambari moja.
Awali, katika hotuba aliyotundika katika mtandao wake wa Truth Social, Rais Donald Trump wa Amerika aliambia raia wa Iran kwamba watapata fursa ya ‘kubadilisha serikali na kujipatia viongozi wapya’ huku akiwataka wasitoke majumbani mwao, kutokana na mabomu ambayo yalikuwa yanyeshe kwenye taifa hilo.
Huku haya yakijiri, hofu imegubika ulimwengu mzima kuhusu hatima ya kisiasa na kiuchumi itakayotokana na vita hivi ambayo wengi wameanza kuviita mwanzo wa Vita Vya Dunia vya Tatu.
Mzozo huu unatarajiwa kuwa na athari kubwa katika bei ya mafuta kutokana mchango wa Iran katika uzalishaji wa mafuta haswa ikiwa mwanachama wa OPEC huku pia ikiwa mdhibiti wa kivukio cha Strait of Hormuz ambacho ni muhimu mno katika usafirishaji wa bidhaa duniani.