Kituo cha polisi kinachotumia mishumaa baada ya kukatiwa stima na maji miaka 2
KITUO cha polisi cha Sameri Park, Kitengela, Kaunti ya Kajiado hakina umeme miaka miwili tangu kianzishwe hali hiyo ikiwalazimu polisi kutumia mishumaa nyakati za usiku.
Mbali na kukosa umeme, kituo hicho kipo katika hali mbaya kimiundomsingi. Kuna meza moja ya mbao ambayo polisi wanaandikia matukio yanavyoripotiwa na ukuta wenyewe nao umepasuka.
Kinaya ni kuwa mradi wa maji wa Tanathi upo tu karibu na kituo hicho ambacho pia hakina bidhaa hiyo muhimu. Umeme na maji hakuna baada ya kukatwa kutokana na bili ambayo haijalipwa.
Hali hiyo sasa imewalazimu polisi kutumia mishumaa na kurunzi nyakati za usiku huku pia hali ya usafi katika kituo hicho ikiwa mbaya.
“Inabidi tujinunulie mishumaa. Maisha yamekuwa magumu sana tunapotekeleza wajibu wetu,” afisa mmoja ambaye hakutaka jina lake linukuliwe aliwaambia wanahabari.
Afisa mmoja alifichua kuwa mshukiwa wa wizi alikuwa amezirai kwenye seli ambayo ni ndogo na hewa haingii vizuri, ikabidi wavunje ukuta kumnusuru.
Kutelekezwa
Wenyeji nao wamesikitishwa na hali mbaya ya kituo hicho cha polisi wakidai kimetelekezwa na jamii ya eneo hilo.
Bw James Okumbu amekashifu uongozi wa eneo hilo kwa kukosa kumakinikia kuboresha kituo hicho.
Anasema ukarabati uliogharimu Sh5 milioni ulioendeshwa na Hazina ya Ustawi wa Maeneobunge (CDF) 2022, haukutosha.
“Tunataka Tume ya Maadili na Kukabili Ufisadi Nchini (EACC) ifanye ukaguzi kufahamu jinsi pesa hizo zilivyotumiwa. Ni miaka miwili baada ya ukarabati kufanyika lakini hatuoni chochote cha maana,” akasema Bw Okumu.
Kamanda wa Polisi wa Kaunti Ndogo ya Isinya Simon Lokitari alikiri kuwa umeme kituoni humo ulikatwa na akasema wajibu wa kulipa gharama hiyo ni wa serikali ya kaunti.
“Licha ya ugumu uliopo, maafisa wetu bado wanajituma sana kutekeleza wajibu wao,” akasema Bw Lokitari.