Habari za Kitaifa

Knec imefilisika, Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali afichua

Na LYNET IGWANDAH March 5th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

BARAZA la Kitaifa la Mitihani Kenya (KNEC), liko katika hali tete kifedha na haliwezi kutimiza wajibu wake wa kifedha bila msaada zaidi kutoka serikali, amesema Mkaguzi Mkuu wa Hesabu, Nancy Gathungu.

Kwa miaka kadhaa sasa, baraza hilo limekumbana na changamoto za kutotengewa bajeti ya kutosha, hali inayosababisha kuchelewa kulipa wafanyakazi wanaohudumu kwa mikataba kufanya kazi wakati wa mitihani ya kitaifa.

Kwa mujibu wa mkaguzi, deni lililolimbikiza la KNEC kufikia Juni 2025, lilikuwa Sh2.79 bilioni, huku madeni yakizidi mali ya sasa ya Sh694.8 milioni.

Baada ya kupitia ripoti za kila mwaka za KNEC, Mkaguzi Mkuu alitangaza baraza kuwa “linafilisika”, akionya kuwa uendelevu wake utategemea msaada wa kudumu kutoka serikali, wadau na wanaolidai.

Viongozi wa KNEC waliambia Kamati ya Bunge kuhusu Utawala na Elimu kuwa, hawana hakika baraza litaendesha shughuli zake, ikitaja ukosefu wa bajeti za kutosha kwa miaka mingi kama chanzo kikuu cha mgogoro wa kifedha.

KNEC iliongeza kuwa suluhisho litaweza kupatikana ikiwa mapendekezo ya kamati kuhusu bajeti ya mitihani yatatekelezwa.

Mkaguzi Mkuu alibainisha kuwa katika hali hii, uongozi wa KNEC hauwezi kutimiza wajibu wake kwa wakati unaotakiwa.

Ufichuzi kuhusu ukosefu wa fedha umejiri wakati maelfu ya walimu waliosimamia mitihani, mameneja wa vituo na waliotahini mitihani ya KCSE na KPSEA 2025 bado wakiwa hawajalipwa.

Mwenyekiti wa chama cha walimu wa shule za sekondari na vyuo Kenya (KUPPET), Omboko Milemba, alitishia kuchukua hatua dhidi ya KNEC kwa kushindwa kulipa walimu.

Waziri wa Elimu, Julius Ogamba alikiri kuchelewa kwa malipo na kuahidi Bunge kuwa serikali inashughulika ili kutoa fedha hizo.