Habari za Kitaifa

Knec yaweka kanuni kunasa wanafunzi wanaofanya lugha ya ishara ili kukwepa Kiswahili

Na WINNIE ATIENO March 10th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

WATAHINIWA wasio na mahitaji maaalum, hawataruhusiwa kujisajili kwa mitihani inayopasa kufanywa na wale wanaoishi na ulemavu, wakati wa usajili kwa Mtihani wa Kitaifa wa Kidato cha Nne (KCSE).

Hii ni baada ya Baraza la Mitihani Nchini (KNEC) kuanzisha kanuni kali za usajili wa watahiniwa kwa mitihani ya KCSE ya mwaka huu na kuzima mtindo ambapo watahiniwa wasio na ulemavu wowote wanajisajili kufanya mtihani wa somo la Lugha ya Ishara ya Kenya ili kuimarisha nafasi yao ya kupata gredi nzuri.

Wanafunzi wenye mahitaji maalum, wakiwemo wenye matatizo ya kuona, akili taahira na ulemavu wa kimwili hufanya mitihani tofauti na wenzao wasio na aina zozote za ulemavu.

Katika mtihani wa KCSE wa 2025, watahiniwa 3,493 walisajiliwa kwa mtihani wa somo la Lugha ya Ishara ya Kenya (KSL) ilhali hawakuhitimu kwa mtihani huo.

KSL huchukuliwa kama somo la kuwawezesha, hawa wanafunzi viziwi, kufidia nafasi ya Kiswahili, inayowapa changamoto wanafunzi wenye aina hiyo ya ulemavu kutokana na sifa zake za kifonetiki.

Hata hivyo, wanafunzi wengi wasio viziwi waliamua kujisajili kufanya mtihani wa somo la KSL, wakitarajia kukwepa changamoto za Kiswahili.

Hii ilichangia wao kuvunjika moyo walipogundua kuwa alama walizopata katika karatasi ya KSL hazikujumuishwa kukadiria gredi yao katika matokeo ya KCSE.

Maafisa wa KNEC walisema kuwa makosa hayo yaligunduliwa na kushughulikiwa na watahiniwa ambao hawakuhitimu hawakupewa gredi katika karatasi za watahiniwa wenye mahitaji maalum.

Katika barua iliyotumwa kwa wakurugenzi wa elimu katika kaunti ndogo, na ambayo Taifa Leo iliona, KNEC imeorodhesha kanuni mpya inayolenga kuhakikisha kuwa ni watahiniwa waliohitimu pekee wanajisajili kwa mitihani inayokusudiwa kufanywa na wanafunzi wenye aina mbalimbali za ulemavu.

Mojawapo ya hitaji ni ithibati ya kimatibabu kuhusu mtahiniwa.

“Data itakayowasilishwa sharti iwe sahihi na zisiwe na makosa ya kitahajia na majina ya watahiniwa yaorodheshwe namna yalivyo kwenye cheti cha KCPE, jinsia, mwaka wa kuzaliwa, uraia, nambari maalum (kwa watahiniwa wa kwanza au waliorudia), nambari ya vyeti vya kuzaliwa na picha za nyuso,” akasema afisi mkuu mtendaji wa KNEC Dkt David Njengere.

Dkt Njengere aliongeza maelezo muhimu kama vile masomo ambayo kwayo mtahiniwa anajisajili, kategoria ya hitaji maalum, ithibati hitajika ya kimatibabu, sharti yanaswe kwa usahihi kwa misingi ya kiwango cha upofu, kutosikia, akili taahira na ulemavu mwa kimwili.

Watahiniwa wenye mahitaji maalum (ulemavu) sasa wanahitajika kuwasilisha stakabadhi hitajika kama, ripoti ya kimatibabu ya hivi punde kutoka kwa daktari anayetambuliwa, ripoti ya ukaguzi kutoka kwa Afisi ya Mahitaji Maalum katika Kaunti Ndogo (EARC), picha kamili yenye rangi ya mtahiniwa mwenye ulemavu wa kimwili na ripoti kutoka kwa mwalimu mkuu hatua zozote maalum zinazopasa kuchukuliwa kuhakikisha usimamizi mzuri wa mitihani.