Lagat hatimaye akanyaga kando kupisha uchunguzi wa mauaji ya Ojwang
BAADA ya kuwekewa presha na Wakenya wa matabaka mbalimbali, hatimaye Naibu Inspekta Jenerali Eliud Lagat amejiondoa kwa muda kutoa nafasi kwa uchunguzi unaoendelea kuhusu kifo cha mwalimu na bloga Albert Ojwang.
Kwenye taarifa aliyoitoa Jumatatu, Juni 16, 2025, Bw Lagat alisema amechukua hatua hiyo kwa kutambua wajibu wake kama Naibu Inspekta Jenerali katika Huduma ya Kitaifa ya Polisi (NPS) na “kwa sababu uchunguzi unaoendelea kuhusu kifo cha kusikitisha cha Albert Ojwang.”
“Leo nimeamua kujiondoa kutoka afisi ya Naibu Inspekta Jenerali wa Polisi hadi uchunguzi unaoendelea utakapokamilika. Majukumu ya afisi yangu kuanzia sasa yatatekelezwa na naibu wangu hadi uchunguzi utakapokamilika,” akasema.
Bw Lagat aliahidi kutoa usaidizi wowote ambao wachunguzi watahitaji watakapokuwa wakiendesha kazi yao.
“Natoa risala za pole kwa familia ya Albert Ojwang’ kwa kupoteza mpendwa wao,” akasema.
Ojwang alikufa Juni 8, 2025 baada ya kupigwa na kuteswa mikononi mwa polisi katika kituo cha polisi cha Central, Nairobi.
Mwanablogu huyo, ambaye pia alikuwa mwalimu, alikamatwa nyumbani kwao Homa Bay, baada ya Bw Lagat kuwasilisha malalamishi kwa Idara ya Upelelezi wa Jinai (DCI) kwamba aliweka mitandaoni taarifa za kumharibia jina.
Kifo cha Ojwang’ kimekasirisha umma haswa baada ya ripoti ya mwanapatholojia wa serikali kufichua kuwa alikufa baada ya kuteswa, kuchapwa kikatili na kunyongwa akiwa kizuizini.
Tangu wakati huo, watetezi wa haki za kibinadamu, wanasiasa na raia wa kawaida wamekuwa wakishinikiza kwamba Bw Lagat ajiuzulu kuhusiana na kifo cha baba huyo wa mtoto mmoja.