Machozi wafanyakazi wa Raila wakifutwa
MACHUNGU, kilio na huzuni vilitawala mkutano wa wafanyakazi wa aliyekuwa kiongozi wa ODM, Raila Odinga, ambapo mabadiliko makubwa ya wafanyakazi yalifanyika katika ofisi ya Capitol Hill, Nairobi, Jumatano, miezi mitano baada ya kifo chake.
Mkutano huo uliojaa hisia uliwaleta pamoja wasaidizi wa muda mrefu waliokuwa uti wa mgongo wa kisiasa wa Odinga kwa miaka mingi.
Wengi walimsaidia kiongozi huyo wa upinzani katika mizunguko kadhaa ya uchaguzi, migogoro ya kisiasa na mabadiliko ya muungano yaliyoamua historia ya kisiasa nchini Kenya.
Hata hivyo, mkutano wa kawaida wa wafanyakazi uligeuka kuwa mgogoro wa kipekee pale baadhi ya wafanyakazi waliambiwa hawahitajiki tena.
Miongoni mwa waliotakiwa kuondoka ni aliyekuwa dereva wa muda mrefu wa Odinga, Philip Juma, aliyefahamika vizuri ndani ya safari za kisiasa za waziri mkuu huyo wa zamani, na kupitia baadhi ya nyakati ngumu za kisiasa nchini. Bw Juma alikuwa afisa wa zamani wa magereza Kenya ambaye alikuwa miongoni mwa watu wa karibu na Odinga.
Wafanyakazi waliokuwa kwenye mkutano walisema kulikuwa na huzuni kubwa na machozi yalitoka pale ukweli wa mabadiliko ulipoanza kueleweka.
Mkutano huo uliitishwa kupitia barua iliyoandikwa Machi 5 na mkuu wa wafanyakazi wa Raila, Andrew Mondo. Mondo pia alihudumu kama Mkuu wa Wilaya ya Kisumu na baadaye kama Mkuu wa Wafanyakazi wa Odinga alipokuwa waziri mkuu.
Hata hivyo, Mondo alihusishwa katika mabadiliko yasiyotarajiwa. Akizungumza na Taifa Leo, Mondo alisema hakujua maelezo kamili kuhusu wafanyakazi waliokuwa wakiondolewa.
“Nimekuwa mgonjwa,” alisema katika mahojiano mafupi ya simu.
Mabadiliko haya yalitokea wakati ODM inakabiliana na mgogoro wa ndani unaotajwa kama mkubwa zaidi tangu kuanzishwa kwa chama hicho miaka ishirini iliyopita, ukihusisha mirengo ya “Linda Ground” na “Linda Mwananchi.”
Wachambuzi wa ndani wanasema kwamba, ikiwa tofauti hizi hazitatatuliwa haraka, zinaweza kuwa changamoto kubwa kisiasa kwa chama.
Hata kabla ya kutatua mgawanyiko wa Linda Ground-Linda Mwananchi, chama kimeanza mchakato wa kurekebisha mtandao wa wafanyakazi wa Odinga, baadhi wakiambiwa kuwa huduma zao hazitahitajika tena baada ya kifo cha kiongozi huyo.
Kulingana na Oduor Ong’wen, Mkurugenzi Mtendaji wa ODM, wafanyakazi waliopo kwenye mishahara ya chama wanaendelea kupokea ujira wao, huku waliokuwa chini ya Odinga binafsi wakiathiriwa.
Idadi ya wahusika ni ndogo, watano hadi saba, kutoka kwa mkuu wa wafanyakazi hadi wasimamizi wa ofisi.
Nje ya mifumo rasmi, Odinga pia alikuwa akisaidia kimya kimya mamia ya watu nchini kila mwezi.
Wengi walikuwa wafuasi wa zamani, washirika wa kisiasa wa muda mrefu, marafiki wa baba yake marehemu Jaramogi Oginga Odinga, marafiki wa utotoni au waliokuwa na mahitaji ya matibabu.
Ben Ombima, mwanasiasa wa ODM, alisema kuwa wafuasi wengi waliokuwa wakitegemea msaada wa binafsi wa Odinga sasa wanakabiliwa na hali ngumu, huku baadhi wakiteseka kutokana na gharama za matibabu.
Mabadiliko haya yametokea pia baada ya kuteuliwa kwa Oburu Oginga, kaka mkubwa wa Odinga, kama kiongozi mpya wa ODM, ambaye ameanzisha ofisi mpya Riverside Nairobi na kuteua Mike Agwanda kuwa mkuu wa wafanyakazi.
Hata hivyo, uteuzi wake umeibua mashaka baadhi ya wanachama wakidai kuwa Agwanda ni mgeni kwenye mifumo ya chama, huku wengine wakisema hakuwa sehemu ya ODM awali na alikuwa mkosoaji wa chama katika sehemu za Nyanza.
Kwa wafanyakazi wa muda mrefu waliokutana Capitol Hill, mkutano wa Jumatano ulikuwa zaidi ya zoezi la kiutawala. Ulikuwa kipindi cha maumivu ya kuondoa mfumo uliotengenezwa kwa miongo kadhaa kuzunguka mojawapo ya wanasiasa wenye ushawishi mkubwa nchini Kenya.
Huku baadhi ya wafanyakazi wakipakia mali zao binafsi na kuondoka, wengi walihisi kuwa kipindi cha uongozi wa ODM chini ya Raila Odinga kimeanza kufikia mwisho.
Huku baadhi ya walinzi wa Odinga wakiajiriwa na Dkt Oginga, Maurice Ogeta alipata kazi mpya kama Mshauri wa Masuala ya Usalama wa Kaunti ya Mombasa aliyoajiriwa na Gavana Abdulswamad Nassir, ambaye pia ni kiongozi mwenza wa ODM.
Ogeta alihudumu kama mlinzi wa Odinga kwa miaka 18, akimpeleka katika kampeni, mikutano na maeneo hatari, pamoja na kuwa naye India alipofariki mwaka jana Oktoba 15.