Habari za Kitaifa

Magavana wakaa ngumu mzozo na maseneta ukichacha

Na NDUBI MOTURI April 1st, 2026 Kusoma ni dakika: 2

MAGAVANA jana walifufua madai ya ufisadi dhidi ya maseneta baada ya Gavana wa Nairobi Johnson Sakaja kukamatwa, na kuzidisha mgogoro kati ya serikali za kaunti na Seneti kuhusu uangalizi.

Mwenyekiti wa Baraza la Magavana (CoG), Gavana wa Wajir, Ahmed Abdullahi, alisema hatua ya kumkamata Bw Sakaja kuhusu kukosa kujitokeza mbele ya Kamati ya Seneti kuhusu Uhasibu wa Pesa za Umma (CPAC) haikufaa kamwe.

Alihoji kwamba mgogoro huo haukuhusu gavana mmoja bali uamuzi wa pamoja uliofanywa na wakuu wa kaunti kufuatia alichotaja kuendelezwa kwa visa vya upunjaji, kuhangaishwa na kutishiwa na baadhi ya wanachama wa kamati.

“Hii haihusu gavana mmoja. Ni msimamo wa pamoja wa Baraza, unaotokana na mtindo wa kufyonza, kuhangaisha pasipo sababu na kutishiwa na baadhi ya wanachama wa kamati,” alisema.

Jaribio la ukamataji lilijiri baada ya magavana kususia kufika mbele ya Kamati, wakisubiri masuala yaliyozuka kuhusu mienendo ya baadhi ya maseneta yasuluhishwe.

Bw Abdullahi alisema magavana 29 waliagizwa kufika mbele ya kamati, lakini ni wawili tu waliohudhuria na wakakataa kuendelea na vikao kuambatana na msimamo wa Baraza.

Alisema baraza liliitisha kikao na uongozi wa Seneti kuangazia masuala husika bila mafanikio.

“Tumeomba kukutana na uongozi wa Seneti kusuluhisha masuala haya lakini hakuna hatua imechukuliwa,” alisema.

Aidha, alisaili matumizi ya polisi kutekeleza amri za Seneti, akionya kwamba hatua hiyo inatishia kuhujumu utawala wa kisheria.

“Tunahimiza Afisi ya Inspekta Jenerali wa Polisi kubaini uzito wa masuala haya ili kuepuka kuvuruga haki au kutumiwa kuendeleza maslahi ya kisiasa na kibinafsi,” alisema Bw Abdullahi.

Aliitisha kuondolewa mbali kwa vibali vyovyote vya ukamataji au mikakati ya ushawishi dhidi ya magavana kusubiri mvutano huo usuluhishwe.

Bw Abdullahi alihoji kuwa kuendesha ukamataji ilhali madai dhidi ya wanakamati yangali hayajasuluhishwa kunakiuka azma ya uangalizi na kunatishia kuzidisha kukosa kuaminiana kati ya seneti na serikali za kaunti.

“Uamuzi wa kufuatilia kukamata magavana wakati madai dhidi ya wanakamati bado hayajasuluhishwa unakiuka lengo la uangalizi, unazidisha kutiliana shaka na kuhujumu utawala wa kisheria,” alisema.

Alisisitiza kuwa magavana wamejitolea kuhusu uwajibikaji na mchakato unaofaa lakini wanapinga alichotaja kuwa utekelezaji wa kibaguzi.

“Tungali tumejitolea kuhusu uwajibikaji, uwazi, utawala wa sheria na mchakato unaohitajika kuambatana na Katiba,” alisema.

Bw Abdullahi alisema maseneta wametumia mara kadhaa mamlaka waliyotwikwa ya idara ya mahakama wakiamuru magavana kujiwasilisha kwao lakini akazua maswali kuhusu tabia yao.

“Tulikumbushwa kila mara kwamba Seneti ina mamlaka ya jaji wa Mahakama Kuu anapotoa amri. Umewahi kuona jaji akiwa na tabia ya baadhi ya maseneta hawa? Iwapo unataka kupatiwa heshima ya jaji ni sharti uwe na mienendo kama ya jaji kortini.”