Habari za Kitaifa

Mahakama yaamuru kosa la ‘kufanya usumbufu wa kuvuruga amani’ lifutwe

Na SAM KIPLAGAT February 13th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

MAHAKAMA Kuu imefuta kifungu cha Sheria ya Kanuni ya Adhabu kinachounda kosa la “kuzua vurugu kwa namna inayoweza kusababisha ukosefu wa amani,” ikisema kuwa kinakiuka Katiba.

Mahakama ilisema kuwa kifungu cha 95(1)(b) cha Kanuni ya Adhabu hakiko wazi na hakieleweki vya kutosha, na kuamuru polisi kusitisha utekelezaji wake mara moja.

Kosa hilo lilikuwa ni miongoni mwa makosa madogo ya uhalifu na adhabu yake ilikuwa ni kifungo cha hadi miezi sita jela.

Chama cha Wanasheria nchini (LSK) kilifanikiwa kupinga kifungu hicho kikidai kuwa ni “cha kikoloni” na kinakiuka haki ya uhuru wa kujieleza kama ilivyolindwa na Katiba, na kwamba kosa hilo limeundwa kwa hali inayoruhusu tafsiri kiholela.

“Inaamuliwa kwamba kifungu cha 95(1)(b) cha Kanuni ya Adhabu hakiwiani na Katiba na kwa hivyo ni batili na hakina nguvu kisheria,” ilisema mahakama.

Mahakama pia ilifuta mashtaka ya jinai yaliyokuwa yamewasilishwa dhidi ya mwanaharakati Morara Kebaso kuhusiana na shughuli zake za kufuatilia miradi ya serikali.

Bw Kebaso alikamatwa Oktoba 8 mwaka jana na kuzuiliwa katika Kituo cha Polisi cha Lang’ata kabla ya kufahamishwa kwamba angefunguliwa mashtaka ya kusababisha vurugu kwa namna inayoweza kusababisha ukosefu wa amani.

Baadaye aliachiliwa kwa dhamana akisubiri kufikishwa katika Mahakama ya Kibera kujibu mashtaka.

LSK ilieleza mahakama kuwa kosa la “kuzozana au kwa namna nyingine kusababisha vurugu zinazoweza kuharibu amani” halilingani na mamlaka ya wananchi wa Kenya, kwa kuwa linawalinda maafisa wa serikali dhidi ya ukosoaji, linazuia mjadala wa masuala ya umma na haliruhusu utetezi wa ukweli.

Mahakama iliambiwa kuwa kifungu hicho ni masalia ya kikoloni kilichoanzishwa wakati wa hali ya hatari miaka ya 1960 ili kuzima upinzani dhidi ya serikali ya kikoloni.

Aidha, utawala wa chama kimoja wa Kanu uliitumia sheria hiyo kukandamiza wakosoaji wakati wa kesi za Mwakenya.

LSK ilisema kuwa kifungu hicho hakisawazishi haki zilizolindwa katika Mswada wa Haki na masharti ya kifungu cha 24 cha Katiba bali kinavunja haki hizo kwa njia isiyo ya haki katika jamii ya kidemokrasia.

Kwa mujibu wa LSK, kifungu hicho kinakiuka uhuru wa kujieleza kwa kuhalalisha adhabu kwa matamshi yasiyohusiana moja kwa moja na mipaka iliyoainishwa katika Ibara ya 33(2) ya Katiba, kama vile propaganda za vita, kuchochea vurugu au matamshi ya chuki.

LSK iliongeza kuwa kifungu hicho kinakiuka kanuni ya uhalali katika Ibara ya 50(2)(n), inayotaka sheria za jinai ziwe wazi na sahihi, hasa pale zinapopunguza haki za kimsingi.

“Hivyo basi, kifungu hiki kinatoa nafasi kubwa mno ya tafsiri ya kibinafsi, ya kupotosha na matumizi mabaya katika kuamua adhabu za jinai,” LSK ilieleza.