Mahangaiko ya polisi aliyefutwa kazi baada ya pesa za Ruto kuibwa kwenye ndege
BW Samuel Wanyoike alikuwa tu ameajiriwa na Huduma ya Polisi wa Utawala mnamo Julai 2007 na kutumwa Garbatulla, Kaunti ya Isiolo.
Mojawapo ya majukumu yake ya mwanzo ya ulinzi ilikuwa mkutano wa kampeni wa chama cha ODM uliokuwa umeandaliwa eneo hilo.
Mbunge wa Eldoret Kaskazini wakati huo na mmoja wa waanzilishi wa ODM William Ruto alikuwa miongoni mwa viongozi waliokuwa wakimpigia debe Raila Odinga, aliyetarajiwa kumenyana na Rais Mwai Kibaki katika uchaguzi wa urais miezi minne baadaye.
Dkt Ruto alikuwa amewasili kwa helikopta.
Ndani yake kulikuwa na vifurushi vya pesa ambavyo thamani yake haijawahi kufichuliwa hadi leo.
Wakati Dkt Ruto na viongozi wengine wa ODM walipokuwa wakihutubia wakazi kundi la wezi jasiri liliingia kwenye helikopta hiyo na kutoroka na fedha hizo na hadi leo, bado haijulikani pesa hizo zilikuwa za nani.
Maafisa wa mawasiliano wa Dkt Ruto hawakujibu maswali kuhusu tukio hilo.
Wanyoike anasema kwamba katikati ya mkutano aliamua kwenda karibu na helikopta hiyo kuichunguza kwa karibu.
Lakini koplo aliyekuwa akilinda helikopta alimzuia na kumpa bahasha ya kahawia kuiweka, akimweleza kuwa ilikuwa na posho za maafisa waliokuwa kazini siku hiyo.
“Nilipewa pesa hizo kwenye bahasha ya kahawia na mkuu wangu ambaye wakati huo alikuwa koplo. Aliniambia ni za kulipa maafisa waliokuwa kazini,” alisema Wanyoike.
Kukubali kubeba bahasha hiyo kulikuwa mwanzo wa mwisho wa kazi yake ya polisi na mwanzo wa vita ya miaka 18 ya kutafuta kurejeshwa kazini.
Baada ya tukio hilo, helikopta ilipoondoka iligunduliwa kuwa fedha zilikuwa zimepotea na ikaelekezwa kurejea Garbatulla mara moja.
Wanyoike wakati huo alikuwa amehifadhi bahasha ndani ya jiko la chuma katika kambi ya AP bila kujua kuwa tayari alikuwa kwenye shida.
Anasema alihojiwa na watu waliovaa suti, wakampekua lakini hawakugusa jiko hilo alilokuwa ameficha pesa.
Baada ya muda mfupi, alikamatwa na kupelekwa Kituo cha Polisi Isiolo.
Hakufunguliwa mashtaka mahakamani, lakini baadaye alifutwa kazi kupitia barua fupi mnamo Septemba 1, 2007, akishutumiwa kwa kuhusika na wizi wa fedha kutoka helikopta, tuhuma anazokanusha hadi leo.
“Nilijiuliza, kama mimi ndiye niliyeiba, kwa nini maafisa waliokuwa wakilinda helikopta hawakukamatwa?” alisema.
Mara baada ya kufutwa kazi, Wanyoike alianza vita ya muda mrefu ya kutafuta haki na kurejeshwa kazini, akisema kuwa hakuwahi kupata haki ya kusikilizwa wala kuonyeshwa ushahidi.
Mwaka 2025, Huduma ya Polisi ilisema uamuzi wa kumfuta kazi ulifanyika chini ya katiba ya zamani na hauwezi kufunguliwa upya.
Kwa Wanyoike, tukio hilo la Garbatulla limebaki kuwa jeraha lisilopona lililoacha maswali mengi.