Habari za Kitaifa

Makadinali waanza kupiga kura ya kuchagua Papa mpya

May 7th, 2025 Kusoma ni dakika: 2

VATICAN CITY

MAKADINALI 133 kutoka sehemu mbalimbali duniani wamejumuika jijini Vatican kushiriki shughuli muhimu ya kumchagua Papa mpya atakayemrithi Papa Francis aliyeongoza Kanisa Katoliki kwa miaka 12.

Mkutano huo maarufu kama conclave umeanza katika kanisa dogo la Sistine ambapo makadinali watabaki hadi pale papa mpya atakapochaguliwa.

Mkutano huo wa makadinali ni muhimu sana kwa waumini bilioni 1.4 wa kanisa Katoliki kote duniani.

Makadinali hao ambao wote wako chini ya umri wa miaka 80 wanatarajiwa kumchagua kiongozi ambaye atakuwa na uwezo wa kukabiliana na changamoto zinazoibuka katika kanisa hilo.

Miongoni mwa changamoto hizo ni mgawanyiko ndani ya kanisa na kutatua madai ya kashfa za ngono.

Kabla ya kuanza rasmi kwa shughuli hiyo, makadinali Jumatano, Mei 7, 2025 walishiriki katika sherehe ya mwisho ya umma ambayo ni misa maalum katika Kanisa Kuu la Mtakatifu Petro wakiongozwa na mkuu wa makidanali Giovanni Battista Re.

Hiyo ndiyo mara yao ya mwisho kuonekana hadharani kabla ya shughuli ya faragha kuanza.

Papa mpya anafaa kupata angalau kura 89 ambazo ni thuluthi tatu.

Kwa siku kadhaa, makadinali wamejadili matarajio yao juu ya papa mpya wakiangazia masuala ya usimamizi wa kifedha, nafasi ya wanawake katika kanisa Katoliki na pia kushuka kwa idadi ya mapadre.

Miongoni mwa wale wanaopigiwa debe ni Pierbattista Pizzaballa kutoka Italia, Peter Erdo kutoka Hungary, na Malcolm Ranjith kutoka Sri Lanka.

Kwa mujibu wa yule atakayechaguliwa, mwelekeo wa Papa Francis wa kuleta mageuzi kwa ajili ya kujumuisha wote utaendelezwa au kubadilishwa.

Msemaji wa Uongozi wa kanisa katoliki la Argentina Maximo Jurcinovic alisema, “Kanisa halitafuti mfano wa Papa Francis wala mrithi wake lakini mrithi wa Petero Mtakatifu. Kwa ajili hii, sote tuna matumaini kwamba baadhi ya mambo ya Papa Francis yataendelezwa.

“Nadhani watu wanahisi hivyo kama ilivyoshuhudiwa kwenye matukio Argentina wakati wa mazishi yake. Tunataka kanisa linalowajali maskini na linalohubiri imani yetu.”

Mtazamo huu wa Jurcinovic unathibitisha umuhimu wa zoezi hilo la kumchagua papa mpya ambapo makadinali watazingatia masuala nyeti.

Ikumbukwe kuwa zaidi ya asilimia 80 ya wakataoshiriki katika uchaguzi huo ni makadinali aliowateua Papa Francis ambaye alikuwa papa wa kwanza kuchaguliwa kutoka Amerika Kusini.

Wengi wao walitokea Afrika na bara Asia.

Raundi ya kwanza ya kupiga kura inafanyika Jumatano jioni.

Baada ya kuchaguliwa kwa Papa mpya, moshi mweupe utatokea kwenye mvuke wa kanisa la Sistine ishara kuwa papa mpya amepatikana.

Ishara ya moshi mweusi itamaanisha papa hajapatikana.

Lakini moshi mweupe bila shaka utawasisimua waumini waliopiga kambi katika bustani la mtakatifu Petero kwamba papa mpya amechaguliwa.

Shughuli hiyo haina muda mahususi hata iliwahi kuchukua miaka mitatu katika karne ya 12.

Ila katika kumchagua Papa Francis mwaka wa 2013, ilichukua siku moja tu.