Habari za Kitaifa

Mama Ngina na Criticos warejea kortini kupigania shamba Taita Taveta

Na JOSEPH WANGUI March 12th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

ALIYEKUWA Mama wa Taifa Mama Ngina Kenyatta pamoja na aliyekuwa Mbunge wa Taveta, Basil Criticos wamerejea mahakamani wakitaka maafisa wa ardhi waamriwe kukamilisha kuhamisha umiliki wa shamba la ekari 2,624 lililoko Kaunti ya Taita Taveta kwa majina yao.

Katika kesi iliyowasilishwa katika Mahakama ya kutatua mizozo ya ardhi na mazingira jijini Nairobi, wawili hao wanasema Msajili Mkuu wa Ardhi amepuuza amri ya mahakama iliyotolewa Desemba 11, 2025 iliyomtaka kutoa cheti cha umiliki wa ardhi hiyo na kufuta rekodi haramu zilizoingizwa katika sajili ya ardhi.

Wanaomba mahakama imwite msajili huyo binafsi aeleze kwa nini maagizo ya awali ya mahakama hayajatekelezwa.

Hata hivyo, mahakama ilikataa kuidhinisha kesi hiyo kama ya dharura na ikaagiza walalamishi kuwakabidhi washtakiwa, akiwemo Mwanasheria Mkuu na Msajili Mkuu wa Ardhi, stakabadhi za kesi ambao walipewa siku 15 kuwasilisha majibu yao.

Mzozo huo wa kisheria unahusu ardhi inayojulikana kama LR 10287/7 katika eneo la East Taita Township.

Ardhi hiyo imekuwa kitovu cha mzozo wa muda mrefu wa umiliki unaohusisha watu binafsi, taasisi za serikali na masuala ya makazi ya walowezi.

Katika kesi yao ya hivi karibuni, wanasema serikali imeshindwa kutekeleza uamuzi wa mahakama uliotolewa Desemba mwaka jana uliothibitisha haki yao ya kumiliki ardhi hiyo.

Wanataka mahakama iamuru msajili wa ardhi kuchapisha katika Gazeti Rasmi la Serikali kufutwa kwa hati haramu za umiliki zilizotolewa kwa ardhi hiyo na pia kuwasilisha ripoti inayoonyesha kuwa amri ya mahakama imetekelezwa.

Katika kiapo chake, Bw Criticos alisema mahakama tayari ilishughulikia suala la umiliki wa ardhi hiyo na kuwaamuru maafisa wa ardhi kuchukua hatua ndani ya muda uliowekwa, ambao sasa umeisha.

“Mshtakiwa wa kwanza, ambaye ni Msajili Mkuu wa Ardhi, amekataa kutoa cheti cha muda cha umiliki au kuwasilisha ripoti ya utekelezaji ndani ya siku 14 licha ya kukumbushwa mara kadhaa,” alisema.

Bw Criticos pia alieleza kuwa mawakili wao waliandikia msajili huyo Desemba 17 na Januari 13 wakimtaka atekeleze uamuzi wa mahakama lakini hawakupata majibu.