Mapengo ya kisheria ya kushughulikia wafu yafichuka kufuatia miili kuzikwa kisiri Kericho
HARUFU iliwafikia kwanza. Kisha ukweli ukajitokeza. Vijana watatu wachimbaji makaburi—watoto wa mitaani waliolipwa Sh1,000 kila mmoja—walitumia usiku wa Machi 19 kuzikwa miili 32 Makaburini, Kericho.
Wengi wao walikuwa watoto. Hakukuwa na familia, wala viongozi wa dini, wala waombolezaji. Kulikuwa tu na barakoa, gari la serikali, na pesa za kuwanyamazisha.
Siku mbili baadaye, waliingia Kituo cha Polisi cha Kericho na kuvunja ukimya. Ushahidi wao ulisababisha mahakama kuagiza ufukuaji wa miili, ambapo watoto 25 walipatikana, huku afisa wa afya wa Kaunti ya Nyamira akikamatwa. Kama wangekaa kimya, miili hiyo ingesalia bila alama, bila kumbukumbu—na kutoweka kabisa.
Tukio la Kericho linaonyesha ukweli mchungu: nchini Kenya, miili hupotea si kwa njama tata, bali kupitia mfumo dhaifu wa kushughulikia wafu unaotokana na hofu, mila na mapengo ya kisheria.
Mnamo 2014, Tume ya Marekebisho ya Sheria ya Kenya ilionya kuwa hakuna mfumo kamili wa kisheria unaoelekeza jinsi ya kushughulikia wafu. Zaidi ya miaka kumi baadaye, hali hiyo bado haijarekebishwa.
Mfano mwingine ni mkasa wa Shakahola, Kaunti ya Kilifi, ambapo zaidi ya miili 429 ilifukuliwa mwaka 2023. Waathiriwa walikuwa wa dhehebu la mhubiri Paul Mackenzie, wengi wao wakifariki kwa njaa, kunyongwa au mateso mengine. Ripoti ya Tume ya Kitaifa ya Haki za Binadamu ilionyesha kuwa polisi walipuuza ripoti za watu waliopotea na ishara za hatari kwa muda mrefu.
Mwaka 2024, miili mingine ilipatikana katika machimbo ya Kware jijini Nairobi, ikiwa imefungwa ndani ya magunia. Baadhi ya waliotambuliwa walikuwa wanawake waliopotea wakati wa maandamano. Hadi sasa, zaidi ya watu 130 hawajulikani walipo kufuatia maandamano hayo.
Chini ya mapengo haya ya kisheria kuna nguvu ya mila. Katika jamii nyingi za Kenya, kushughulikia maiti huonekana kama jambo la kutia najisi au hofu. Familia nyingi huchagua kutoangalia hata miili ya wapendwa wao, na kuachia jukumu hilo wahudumu wa mochari na makaburi.
Hali hii kitamaduni inazaa mazingira ya kutokuwajibika. Wafanyakazi wa makaburi, mochari na hata wale wa kuchoma maiti hufanya kazi katika maeneo ambayo watu wengi huepuka. Hakuna ufuatiliaji wa kutosha, na mara nyingi hakuna mtu anayeuliza maswali.
Hali ni mbaya zaidi katika majengo ya kuchoma maiti. Nchini Kenya, hakuna sajili ya kitaifa ya miili inayochomwa, wala mfumo wa kuhakikisha majivu yanayorejeshwa kwa familia ni ya wapendwa wao.
Katika tukio la Kericho, taratibu zote zilikiukwa. Hakukuwa na vibali sahihi, hakukuwa na uratibu kati ya kaunti, na hakukuwa na ufuatiliaji. Uwajibikaji unasambaratika kati ya serikali za kaunti, mahakama, polisi na taasisi nyingine—hakuna anayebeba jukumu kamili.
Wataalamu wanasema Kenya inahitaji haraka mfumo wa kisasa wa kufuatilia miili: sajili ya kidijitali ya mazishi, ukaguzi wa mara kwa mara wa makaburi, udhibiti wa tanuri za kuchomea maiti, na ulinzi kwa wanaofichua maovu.
Vijana wale watatu waliolipwa Sh1,000 ndio “ulinzi” pekee uliokuwepo. Wao ndio waliovunja ukimya ambao mfumo mzima umejengwa juu yake.
Mpaka sasa, swali linaendelea kubaki: nani anasimamia makaburi? Na jibu, licha ya miaka yote kupita na miili mingi kupatikana, bado ni lile lile, hakuna yeyote.