Habari za Kitaifa

Maraga akemea kukamatwa kwa Rose Njeri aliyebuni tovuti ya kupinga Mswada wa Fedha

Na CHARLES WASONGA June 2nd, 2025 Kusoma ni dakika: 2

ALIYEKUWA Jaji Mkuu David Maraga ameishutumu serikali kufuatia kukamatwa kwa mwanaharakati Rose Njeri, akisema hatua hiyo inaboronga umuhimu wa Madaraka Dei.

Kwenye taarifa aliyoitoa Jumapili asubuhi, Juni 1, 2025, Bw Maraga alisema kukamatwa kwa Njeri saa chache kabla maadhimisho ya siku ambayo Kenya ilipata uhuru wa kijitawala kidemokrasia ni dharau kwa moyo wa siku hii.

“Bi Rose Njeri ndiye wa hivi punde kutekwa nyara kwa madai ya kuvumbua jukwaa la kidijitali la kuwawezesha rais kutoa maoni yao kuhusu Mswada wa Fedha wa 2025. Hii ni kinyume kabisa na moyo wa Madaraka Dei,” Bw Maraga akasema.

Njeri, ambaye pia ni mtaalamu wa utengenezaji wa programu za kidijitali, aliripotiwa kukamatwa Ijumaa alasiri katika mtaa wa South B, Nairobi na kupelekwa katika kituo cha Polisi cha Pangani ambako anazuiliwa.

Jukwaa lake la kimtandao kwa jina “Civic Email”, kiliwezesha raia kutuma kwa urahisi pingamizi zao kwa wabunge kuhusu mapendekezo tata yaliyomo kwenye Mswada wa Fedha wa 2025.

Kuzuiliwa kwake—bila kufunguliwa mashtaka au kupewa dhamana— kumepingwa vikali na makundi ya kijamii, waharakati wa kutetea hadi za kidijitali na makundi ya vijana kote nchini.

Kwenye taarifa yake, Bw Maraga alilalamikia mwenendo wa serikali kuwanyima vijana uhuru wa kujieleza akisema kitendo hicho kinahujumu juhudi za kukuza utawala wa kidemokrasia nchini.

“Vijana hawana cha kusherehekea katika Madaraka Dei ya mwaka huu,” akaeleza.

“Ukosefu wa ajira ungali kero kubwa nchini, nafasi za watu kujitafutia pato zinapungua, huku wanasiasa matajiri wakiishi kwa utajiri kupindukia. Inakera kwamba idadi kubwa ya vijana wanaishi kwa uchochole,” Bw Maraga akaeleza.

Huku sherehe za kitaifa za Madaraka Dei zikiadhimishwa katika uwanja wa Raila Odinga, mjini Homa Bay, Jaji huyo Mkuu mstaafu alihimiza serikali kuendeleza maadili ya haki na uhuru.

“Taifa linahitaji kufufua moyo halisi ya Madaraka,” akaeleza huku akishauri Wakenya kutumia mwezi huu wa Juni kuwakumbuka zaidi ya vijana 60 waliokufa mwaka jana wakati wa maandamano ya Gen Z.

“Huu ni mwezi ambapo Wakenya wote wanapaswa kuwaenzi na kusimama na wale waliojeruhiwa na kutekwa nyara na kuziliwaze familia za wale waliopoteza wapendwa wao kutokana na ukatili wa polisi,” akasema.