Habari za Kitaifa

Masaibu ya Wakenya waliokwama vitani hofu ikiendelea kutanda Uarabuni

March 3rd, 2026 Kusoma ni dakika: 3

WAKENYA wanaoishi katika nchi za Ukanda wa Mashariki ya Kati wameelezea hofu yao huku vita vikichacha eneo hilo, wengi wao wakihofia usalama wao na athari za vita hivyo.

Baadhi ya Wakenya waliozungumza na Taifa Leo walisema kwa sasa hawafanyi kazi na wameshauriwa kukaa nyumbani.

Wanahisi wamekwama kwa sababu hawawezi kusafiri kurejea nyumbani ikizingatiwa kuwa mikondo mingi ya ndege ya Mashariki ya Kati na eneo la Ghuba imefungwa na ndege kupigwa marufuku kusafiri.

“Tumeshtuka, lakini tupo salama,” alisema Mkenya anayeishi Dubai, Milki ya Kiarabu, akieleza kwamba “kinachotendeka huko kila wakati hufika hapa”.

Mkenya mwingine alisema, “Tunachunguzwa hapa, hivyo siwezi kusema mengi. Tumeambiwa tukae nyumbani hadi maelezo zaidi yatakapotolewa.”

Walichelea vilevile kutuma picha zao wakihofia kuhatarisha usalama wao.

Mwangi*, si jina lake halisi, anayefanya kazi katika shirika la kimataifa la usafiri wa ndege alisema Mashariki ya Kati ingali kituo muhimu cha kusambaza mafuta ulimwenguni na mikondo ya kibiashara kimataifa.

Wameonywa vilevile wasisambaze picha za vituo vilivyoshambuliwa.

Machafuko ya muda mrefu huenda yakatatiza mifumo ya usambazaji bidhaa, kusababisha bei za kawi kupanda na kuathiri uchumi wa nchi zinazoendelea kujikwamua kutokana na shinikizo za mfumko wa bei.

Wakenya wanaoishi eneo hilo vilevile wamekuwa wakichapisha video kwenye mitandao ya kijamii kuonyesha maeneo ambayo yamelengwa kwa makombora au vifusi vilivyoteketezwa na silaha hizo.

Ukanda wa Mashariki ni makao ya maelfu ya Wakenya wahamiaji walioajiriwa katika sekta za kazi za nyumbani, usafiri, ujenzi na nyinginezo.

Familia zao huku Kenya zinasema zinafuatilia kwa makini ripoti za vyombo vya habari na kuwasiliana na wapendwa wao.

“Tumenusurika nyakati ngumu hapo mbeleni. Tuna hofu, ndiyo, lakini tuna matumaini,” akasema Wanjiru*.

Mashambulizi hayo yalijiri huku Iran ikilipiza kisasi dhidi ya shambulizi kubwa lililotekelezwa na Amerika kwa ushirikiano na Israel lililoanza Jumamosi.

Oparesheni hiyo ilimuua kiongozi wa kidini wa Iran, Ayatollah Ali Khamenei, viongozi wengine wakuu wa jeshi, na kulenga vituo vya jeshi na serikali kote Iran.

Shule moja ililengwa vilevile huku watu wasiopungua 148 wakiuawa katika shambulizi hilo.

Kwa kulipiza kisasi, Iran imeshambulia ngome za Amerika katika nchi za UAE, Qatar, Bahrain na Saudi Arabia, mbali na kuishambulia Israel moja kwa moja.

Serikali ya Kenya imehimiza utulivu, ikisema inaangazia hali na kutathmini athari zinazoweza kutokea kiuchumi.

Kenya haijatangaza mabadiliko yoyote ya kisera lakini imeashiria mikakati ya dharura huenda ikatekelezwa iwapo masoko ya kimataifa yatazorota.

Wizara ya Masuala ya Kigeni, kupitia ilani, iliwashauri Wakenya wanaoishi ndani au kusafiri kupitia nchi zilizoathirika kumakinika kuhusu usalama wao.

Ilani hiyo hasa ilikusudiwa raia wa Kenya nchini Iran, Israel, Qatar, UAE, Bahrain, Kuwait, Saudi Arabia, Jordan, Iraq, na maeneo jirani.

Inatarajiwa mapigano hayo yataathiri uchumi wa Kenya kwa sababu taifa hili huagizia bidhaa nyingi za petroli kutoka eneo hilo, hivyo kuiweka kwenye hatari ya kuathiriwa pakubwa na misukosuko kwenye masoko ya mafuta ulimwenguni.

Kwingineko, jana Rais William Ruto alionekana kuegemea mrengo wa Amerika na Israel katika vita vinavyoendelea dhidi ya Iran.

Rais Ruto alituma taarifa ambayo ilishutumu mashambulizi ambayo yanatekelezwa na Iran dhidi ya kambi za kijeshi za Amerika katika Ukanda wa Mashariki ya Kati.

Alikemea mashambulizi ambayo yatekelezwa dhidi ya UAE, Qatar, Saudi Arabia, Iraq, Oman, Kuwait, Jordan na Bahrain.

Kwenye taarifa, Rais Ruto alisema uhasama huo wa kieneo unatishia amani na usalama duniani na kutoa wito kwa pande zote kusaka maelewano.

Hata hivyo, balozi wa Iran nchini, Ali Gholampour, alipohutubia wanahabari jijini Nairobi alisisitiza kuwa uhusiano baina ya Kenya na Iran bado ni thabiti ila akaonekana kumkosoa Rais aliyelaumu Iran.

“Uhusiano wetu unabaki kuwa imara lakini mataifa yote yanapaswa kuzingatia mkataba wa Umoja wa Mataifa (UN) unaohitaji taifa chokozi kukemewa badala ya lililochokozwa,” akasema Gholampour.

Wakati huo vilevile, safari za ndege kuelekea Dubai na Sharjah kwa kutumia ndege la shirika la humu nchini, Kenya Airways, zimesimamishwa “hadi notisi nyingine itakapotolewa”.