Habari za Kitaifa

Mashaka zaidi kwa Tuju polisi wakimshutumu kwa madai ya ‘kujiteka nyara’

Na HILLARY KIMUYU, KEVIN CHERUIYOT March 24th, 2026 Kusoma ni dakika: 3

MASHAKA zaidi yalijiri jana baada ya Waziri wa zamani wa Utalii, Raphael Tuju ambaye alikuwa ametoweka kwa siku mbili, kujitokeza katika makazi yake mtaa wa Karen, Nairobi.

Bw Tuju alijitokeza hadharani jana baada ya kuripotiwa kutoweka mnamo Jumamosi kabla ya kudaiwa kujeruhiwa akiwa katika kituo cha polisi cha Karen.

Kwa mujibu wa familia yake, Bw Tuju na dereva wake walitoweka alipokuwa akienda kushiriki mahojiano katika idhaa ya redio ya Ramogi.

Gari lake baadaye lilipatikana limeachwa katika barabara ya Miotoni, Karen.

Akiongea na wanahabari nyumbani kwake, Bw Tuju alisema alienda mafichoni baada ya kutambua kuna watu fulani waliokuwa wakimfuata Jumamosi.

Alidai gari aina ya Land Cruiser lilikuwa likimfuata bila kuwa na nambari ya usajili ndiposa akaamua kujificha. Alisema haikuwa mara ya kwanza kuliona gari hilo.

“Niliacha barabara niliyokuwa nafuata na kugeukia barabara ya Nandi ndipo wasinifuate kwa sababu wangelazimika kugeuza gari kwanza na hivyo ndivyo niliwatoroka,” akasema Bw Tuju akikumbuka alivyoliacha gari lake na kutokomea.

Alidai kuwa familia moja Kiambu kwenye mpaka wa kaunti hiyo na Nairobi ilimpa hifadhi hadi baada ya saa sita usiku wa kuamkia jana ndipo akarejea nyumbani.

Baada ya kuongea na wanahabari, Bw Tuju alipelekwa katika Kituo cha Polisi cha Karen kuandikisha taarifa, tukio ambalo mawakili wake walisema lilijaa fujo.

Walidai mbunge huyo wa zamani wa Rarieda alinyanyaswa, akapata majeraha na wakasisitiza lazima apelekwe Hospitali ya Karen ili kupokea matibabu.

Naye Mkuu wa Idara ya Upelelezi nchini (DCI) Mohamed Amin alizua utata zaidi kuhusu kutoweka kwa Bw Tuju akidai alikuwa amejificha nyumbani kwake Karen.

Akiongea katika kikao na wanahabari Nairobi, Bw Amin alisema Bw Tuju, alidanganya umma na kusababisha polisi kuzingira boma lake baada ya ripoti kuzuka kuhusu kutoweka kwake Jumamosi.

Bw Amin alisema hatua ya familia kukataa kushirikiana na polisi ilizua shaka kuhusu iwapo katibu huyo wa zamani wa chama cha Jubilee alitekwa nyara kwa ukweli.

“Kutokana na kuwakataza polisi wasiingie makazi yake, tuliwatuma maafisa wa usalama kuyalinda huku uchunguzi ukiendelea huku tukisaka amri ya korti kupekua makazi hayo,” akasema Bw Amin.

Alisisitiza kuwa Bw Tuju hakupotea jinsi umma ulivyofanywa kuamini bali alikuwa amejificha kwenye makazi yake.

“Kutokana na ujasusi na uchunguzi wa DCI nasema haya bila wasiwasi wowote kuwa Bw Tuju, alikuwa kwenye makazi yake kipindi chote ambacho alidaiwa kutoweka. Simu yake ilizimwa mnamo saa 12 jioni na dakika 18 mnamo Machi 21, 2026. Wakati huo alikuwa kwenye makazi yake ya Karen,” akaongeza Bw Amin.

“Alipofahamu kuwa polisi walikuwa wakikaribia kufahamu ukweli na hadaa zake zilikuwa zimefichuliwa, aliamua kujitokeza na kuthibitisha kuwa hakuwa ametekwa nyara bali alijificha tu katika makazi yake.”

Mkuu huyo wa DCI alithibitisha kuwa Bw Tuju amekamatwa baada ya kujitokeza nyumbani kwake.

“Amekamatwa ili aandikishe taarifa kwenye Kituo cha Polisi cha Karen ambapo atafafanua alikokuwa, jinsi alivyoacha gari lake barabarani, mazingira yalisababisha afanye hivyo, ripoti ya familia yake, maelezo ya wasamaria wema aliodai walimsaidia kwa kuwa mwenyeji wao Kiambu,” akasema Bw Amin.

Akiongea Baringo jana, Waziri wa Usalama wa Ndani Kipchumba Murkomen alitaka mahakama ichukue hatua kali dhidi ya Bw Tuju kwa kujiteka nyara.

“Uchunguzi umefichua Tuju alikuwa nyumbani kwake akiwa amejifungia na kuzima simu yake huku kitendo chake kikimzolea huruma kutoka kwa umma. Hivi visa vya kujiteka nyara ni vingi na tukileta mtu aliyejiteka nyara kortini, basi aadhibiwe vikali,” akasema Bw Murkomen.

Wiki moja iliyopita madalali, maafisa wa usalama na kundi la vijana walivamia kampuni ya Dari mtaani Karen, mali ya Bw Tuju na kuuchukua usimamizi wake kutokana na deni la Sh1.19 bilioni la Benki ya EADB. Tukio hilo lilitikisa mawimbi ya kisiasa nchini, viongozi kutoka mirengo mbalimbali ya kisiasa wakifika na kuungana na Bw Tuju kutetea mali yake.

Jana, Kinara wa Wiper Kalonzo na Kiongozi wa DP Justin Muturi ni kati ya vinara wa upinzani ambao walifika kwa Bw Tuju na kukabiliana na maafisa wa usalama wakati ambapo alifikishwa kituo cha polisi cha Karen kuandikisha taarifa.