Mashujaa Dei kuendelea kama kawaida licha ya hofu kwamba ingeahirishwa
SIKUKUU ya Mashujaa itakayoadhimishwa leo, itatumika kumuenzi aliyekuwa Waziri Mkuu Raila Odinga ambaye alizikwa jana.
Bw Odinga alizikwa Kang’o Ka Jaramogi, kando ya babake na karibu na wanafamilia wake katika hafla iliyoongozwa na Rais William Ruto na viongozi wengine wa hadhi ndani na nje ya nchi.
Rais Ruto leo anatarajiwa kuongoza maadhimisho ya leo ambayo yatatumika kumuenzi Raila. Sherehe hizo zitafanyika katika uwanja wa Ithookwe, Kaunti ya Kitui
“Ni vizuri kutambua kuwa siku hii ya Mashujaa itatumika kuwatambua mashujaa wetu na Raila atakuwa kati ya wale ambao watatambuliwa na kuenziwa,” akasema Msemaji wa Serikali Isaac Mwaura.
“Serikali inatoa wito kwa Wakenya wa matabaka mbalimbali wajitokeze kwa maadhimisho ya Mashujaa kama sehemu ya kuendelea kumuezi Raila,” akasema Bw Mwaura.
Alikanusha habari zilizoenea mitandaoni kuwa sherehe hiyo ingeahirishwa kutokana na mauti na mazishi ya Raila.