Habari za Kitaifa

Maswali IEBC ikidaiwa Sh4.2bn na mawakili deni likipanda mwaka usio wa uchaguzi

Na SAMWEL OWINO March 16th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

KAMPUNI kadhaa za uwakili ambazo ziliwakilisha Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka Nchini (IEBC) kortini, zimesema kuwa zinadai tume hiyo Sh4.2 bilioni tangu 2013.

Sasa itabidi IEBC na kampuni hizo ziingie makubaliano jinsi ambavyo pesa hizo zitalipwa.

Kamati ya Haki na Masuala ya Kisheria Bungeni ilisema IEBC lazima iingie maelewano jinsi ambavyo pesa hizo zitalipwa.

“Tutalazimika kuwa na mazungumzo kuhusu ulipaji wa madeni hayo,” akasema George Murugara.

Wakati wa mkutano huo kuhusu bajeti ya ziada, IEBC iliwaambia wabunge hao kuwa imeangazia upya madeni yake na kiwango hicho kimeshuka kutoka Sh5.6 bilioni hadi Sh4.9 bilioni. Pesa za kuwalipa mawakili pia zimepunguzwa hadi Sh402 milioni.

Kaimu Afisa Mkuu Mtendaji wa IEBC Moses Sunkuli aliambia kamati hiyo kuwa kufikia Januari 19, 2026, madeni ya IEBC yalikuwa Sh4,987,566,493 huku pesa za mawakili ikiwa Sh4,273, 019 na huduma nyingine Sh713, 713, 473.

Bw Sunkuli alisema kabla ya ukaguzi wao, deni lao lilikuwa Sh5.6 bilioni lakini sasa shughuli hiyo imepunguza deni hilo kwa Sh402,500,727.

“Tume imekagua madeni yake ambayo msingi wake ni malipo kwa huduma za mawakili na huduma nyinginezo kutokana na chaguzi za miaka ya nyuma,” Bw Sunkuli akawaeleza wabunge.

Mbunge wa Kibwezi Mwengi Mutuse alizua swali kuhusu jinsi ambavyo tume ilipunguza zaidi ya Sh402 milioni akisema baada ya muda pesa hizo zinaweza kushuka zaidi.

“Ndani ya wiki mbili mmeokoa walipaushuru kwa Sh402 milioni, naomba mpate muda zaidi ili kupunguza hela hizi. Kama kampuni hizo zimesubiri tangu 2013 basi zinaweza kusubiri hadi tupitishe bajeti ya 2026/27,” akasema Bw Mutuse.

Kulingana na stakabadhi ya IEBC mbele ya kamati hiyo, deni la tume ilipanda hadi Sh5.6 bilioni mwaka wa kifedha 2022/23 na 2024/25.

Kamati hiyo ilizua maswali jinsi ambavyo deni hilo liliongezeka ilhali miaka hiyo haikuwa ya uchaguzi.

“Mnatuambia kuwa ndani ya mwaka moja pesa za mawakili zilipanda hadi Sh3 bilioni ilhali si mwaka wa uchaguzi? Tunahitaji kuzungumzia hili,” akasema Mbunge wa Rarieda Otiende Amollo.

IEBC ilionya kuwa kukosa kulipwa kwa madeni hayo kwa wakati kutatiza shughuli zake kuelekea uchaguzi wa 2027.