Maswali kuhusu ziara za mgeni mwenye utata kimaadili katika Ikulu
MNAMO Januari 11, mfanyabiashara tata kutoka Zimbabwe, Wicknell Chivayo anayejulikana pia kama “Sir Wicknell”, alisafiri kwa ndege hadi Ikulu ndogo ya Sagana kukutana na Rais William Ruto pamoja na Naibu Rais Kithure Kindiki.
Mfanyabiashara huyo, anayejulikana sana nchini mwake kutokana na hukumu ya awali ya ulanguzi wa fedha, baadaye alichapisha picha katika mitandao ya kijamii akiwapongeza viongozi hao wawili.
Licha ya maswali mengi kuhusu uadilifu wake, Bw Chivayo amekuwa mtu wa kawaida katika ofisi kubwa na zenye mamlaka, akitangamana na watu wenye ushawishi mkubwa.
Katika makala iliyochapishwa na BBC mnamo Juni 22, 2025, alijitaja kama anayefanya kazi kwa bidii.
BBC inasema kuwa kwa miaka mingi, Sir Wicknell, kama anavyojiita, anapenda kujigamba kuhusu utajiri wake kwenye Instagram.
“Ingawa yuko wazi kuhusu jinsi anavyotumia pesa zake, hayuko wazi sana kuhusu jinsi anavyozipata,” ilisema BBC.
Aliitembelea Ikulu ya Nairobi mara kadhaa mwaka jana, na Aprili alikutana na Rais wa Tanzania Samia Suluhu Hassan katika mkutano ulioratibiwa na Rais Ruto.
“Alasiri ya leo, nilipata heshima kubwa tena ya kumtembelea Rais William Ruto Ikulu ya Nairobi. Kila mkutano na Rais ni fursa ya kipekee, kwani kila mara hunipa hekima kubwa kuhusu kuishi maisha yenye maana yanayompendeza Mungu,” alisema katika ujumbe wake wa Mwaka Mpya 2026.
Hata hivyo, upinzani sasa umeibua wasiwasi kuhusu historia yake tata na madai ya kuhusika katika usambazaji wa vifaa vya uchaguzi nchini Afrika Kusini na Namibia.
Haya yanatarajiwa kuzua maswali zaidi huku nchi ikielekea uchaguzi mkuu mwaka ujao.
Upinzani unadai kuwa Bw Chivayo anahusishwa na chaguzi zenye utata nchini Afrika Kusini na Namibia kutokana na madai ya kuhusika kwake katika usambazaji wa vifaa vya uchaguzi.
Malalamishi ya muungano wa upinzani yanafanana na yale yaliyowahi kutolewa na aliyekuwa kiongozi wa Azimio marehemu Raila Odinga kuhusu raia wa Venezuela, Jose Camargo, aliyehusishwa na matokeo ya uchaguzi wa urais wa 2022, kesi ambayo Odinga aliwasilisha bila mafanikio katika Mahakama ya Juu.
Msemaji wa Ikulu, Bw Hussein Mohamed, hakujibu maswali yetu kuhusu kwa nini Rais alikuwa akishirikiana na mtu mwenye historia yenye utata, wala Mkuu wa Mawasiliano ya Rais (PCS), Bw Munyori Buku.
Mkuu wa Waziri na Waziri wa Masuala ya Nje Musalia Mudavadi pia hakujibu maswali yetu.