Habari za Kitaifa

Maswali mkewe Obado akitengewa mgodi wa dhahabu

Na MOSES NYAMORI, GEORGE ODIWUOR February 19th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

OMBI la utawala wa Gavana wa Migori, Ochillo Ayacko, kwa Bunge la Kaunti kuidhinisha ekari 900 za ardhi kwa kampuni inayomilikiwa na familia ya mtangulizi wake Okoth Obado, limeibua maswali huku kukiwa na madai ya mazungumzo ya kisiasa kuelekea uchaguzi mkuu wa 2027.

Baraza la Mawaziri la kaunti hiyo liliidhinisha ombi la ardhi hiyo kutengewa kampuni ya Global Search Solutions Ltd, inayomilikiwa na mke wa Bw Obado, Bi Hellen Odhiambo Odie.

Kampuni hiyo inaomba ikodishiwe shamba hilo linalojulikana kama Muhuru Kadem/Macalder/498 (LR 17955) kwa muda wa miaka 30.

Kwa mujibu wa nyaraka tulizozipata, kampuni hiyo imeeleza kuwa inalenga kufufua kilimo cha pamba na kuanzisha kiwanda cha kusafisha dhahabu kwa kutumia teknolojia ya Carbon in Pulp (CIP).

Bw Ayacko na Bw Obado wamekuwa na historia ndefu ya ushindani mkali wa kisiasa. Hata hivyo, hivi karibuni wawili hao wameonekana kukaribiana, hali inayozua tetesi kuwa huenda gavana huyo wa zamani akawania kiti cha useneta.

Bw Obado tayari amejiunga na chama tawala cha United Democratic Alliance (UDA) kuelekea 2027, huku duru zikisema Gavana Ayacko analenga kuungwa mkono kwa muhula wa pili.

Gavana huyo anakabiliwa na ushindani mkali, hasa kutoka kwa Mbunge wa Uriri, Mark Nyamita, ambaye ametangaza nia ya kumng’oa uongozini katika uchaguzi ujao.

Taifa Leo ilimtafuta Bw Ayacko kuzungumzia uamuzi wa utawala wake na iwapo uhusiano wake wa sasa wa kisiasa na Bw Obado umeathiri hatua hiyo, lakini hakujibu jumbe wala simu zetu kufikia wakati wa kuchapisha habari hii. Ofisi yake ya mawasiliano iliahidi kutoa majibu lakini nayo haikufanya hivyo.

Ardhi inayokusudiwa kukodishwa ni ukanda unaojulikana kwa uwepo wa madini ya dhahabu na hapo awali umekuwa kitovu cha migogoro kati ya wachimbaji madini wa eneo hilo.

Kulingana na rekodi, ardhi hiyo awali ilikuwa mali ya umma iliyoshikiliwa kwa niaba ya wananchi na Halmashauri ya Kaunti ya South Nyanza (sasa Serikali ya Kaunti ya Migori).

Sehemu ya ardhi hiyo kwa sasa ina ofisi za serikali ya kaunti na kitaifa, hospitali ya kaunti ndogo, shule, soko, steji ya mabasi, Eneo la Viwanda na Chuo Kikuu cha Rongo.

Katika kumbukumbu ya Baraza la Mawaziri la kaunti, serikali inasema mradi uliopendekezwa wa kufufua kilimo cha pamba na kuanzisha kiwanda cha kusafisha dhahabu utajumuisha mashamba ya pamba, ofisi za utawala, kiwanda cha kusafisha dhahabu, mabohari, maegesho, eneo la mitambo, ofisi za uhandisi, makazi ya wafanyakazi na kituo cha utafiti — hatua zinazodaiwa kuchochea maendeleo ya eneo hilo, ajira na ukuaji wa nguvu kazi.

Mnamo Desemba 3, 2025, Kiongozi wa Wengi katika Bunge la Kaunti ya Migori, Ken Ouma, aliwasilisha hoja ya kuomba kuidhinishwa kwa hatua hiyo.

Hata hivyo, katika hoja hiyo alitaja ekari 350, ilhali kumbukumbu ya Baraza la Mawaziri inaonyesha ekari 900.

Bw Ouma pia aliomba kuidhinishwa kwa ekari 50 kwa Joymakers Foundation, ekari 50 kwa Vivatel Networks Limited na ekari 31 kwa Noiya Women Enterprises Ltd.