Habari za Kitaifa

Mateso na mahangaiko hospitali za umma matabibu wakigoma kote nchini leo

Na HELLEN SHIKANDA July 30th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

HUDUMA katika hospitali za umma kote nchini zitazorota pakubwa baada ya wauguzi kujiunga na mgomo wa kitaifa ulioanza wiki iliyopita.

Mgomo wao unafanya hali kuwa mbaya wakiungana na wahudumu wengine wa afya wanaosusia kazi.

Mgomo huo sasa unahusisha wauguzi, maafisa wa maabara, maafisa wa afya ya umma, wataalamu wa lishe, wafamasia na maafisa wa utabibu.

Kutokana na hali hiyo, huduma muhimu kama vipimo vya maabara, utoaji wa dawa, ushauri wa lishe, ufuatiliaji wa magonjwa, matibabu ya wagonjwa na huduma za uuguzi zitakwama.

Wagonjwa wengi sasa watalazimika kusubiri kwa muda usiojulikana, kutafuta matibabu katika hospitali za kibinafsi kwa gharama kubwa au kurejea nyumbani bila kutibiwa.

Katibu Mkuu wa Chama cha Kitaifa cha Wauguzi Kenya (KNUNM), Seth Panyako, alisema zaidi ya wauguzi 32,000, bila kujumuisha wale wa Hospitali ya Kitaifa ya Kenyatta (KNH), watagoma kazi.

Alisema wauguzi wa KNH wataanza mgomo wao Julai 31.

Kufikia saa 8:30 mchana Jumatano, kaunti 22 zilikuwa zimethibitisha kuwa wauguzi wao wamegoma, zikiwemo Machakos, Kitui, Kajiado, Kisii, Kisumu, Mombasa, Bungoma, Meru, Murang’a, Siaya, Nyamira, Embu, Lamu, Kwale, Homa Bay na Nyandarua.

Leo, wauguzi wanatarajiwa kufanya maandamano ya amani jijini Nairobi kuanzia Green Park hadi Wizara ya Afya na baadaye katika ofisi za Baraza la Magavana (CoG) Westlands.

Viongozi wa chama hicho wanashutumu Tume ya Mishahara na Marupurupu (SRC) pamoja na Baraza la Magavana kwa kuchelewesha utekelezaji wa makubaliano ya muda mrefu kuhusu maslahi ya wauguzi.

Bw Panyako alisema madaktari na maafisa wa utabibu wameidhinishiwa mikataba yao ya pamoja ya kazi (CBA), lakini madai ya wauguzi yamekuwa yakipuuzwa.

“Madaktari na maafisa wa utabibu wameidhinishiwa CBA zao, lakini kila mara SRC inapambana na wauguzi. Hatujui kama wanawachukia wauguzi au wana tofauti na viongozi wa chama,” alisema.

Naibu Katibu Mkuu wa KNUNM Lucy Mburu alisema Baraza la Magavana lilisitisha mazungumzo bila kutoa maelezo.

“Waliahidi watatupa majibu ndani ya wiki mbili lakini walinyamaza. Tulipofuatilia hata katika ofisi zao hatukupata jibu, ndipo tukatoa notisi ya mgomo ya siku saba,” alisema.

Wauguzi wanataka kukamilishwa kwa CBA ya mwaka 2025-2029 pamoja na utekelezaji wa miongozo mipya ya maendeleo ya taaluma yao.

Bi Mburu alisema bado kaunti nyingi zinatumia mfumo wa mwaka 2014 ambao hauzingatii maendeleo ya taaluma ya uuguzi.

Miongozo mipya inapandisha daraja la kuanzia kazi kutoka kundi la H hadi J na kutambua utaalamu kama wauguzi wa wagonjwa mahututi na wahudumu wa ICU.

Pia wanataka kurekebishwa kwa makubaliano ya kurejea kazini ya mwaka 2017 ili marupurupu yaboreshwe.

Chama hicho kinataka marupurupu ya sare yaongezwe kutoka Sh10,000 hadi Sh25,000, ya huduma za uuguzi kutoka Sh20,000 hadi Sh30,000 na ya hatari kutoka Sh3,850.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa SRC Sammy Chepkwony alisema tume iko tayari kukutana na viongozi wa wauguzi kutafuta suluhu.

Alisema mzozo kuhusu CBA ya 2025-2029 uko mbele ya mpatanishi chini ya Wizara ya Kazi na ana matumaini utatatuliwa kwa maelewano.

Katika Kaunti ya Homa Bay, viongozi wa KNUNM walionya kuwa wataitisha mgomo ikiwa serikali ya kaunti haitatekeleza makubaliano ya awali ya kurejea kazini.

Katika Nyandarua, Katibu wa chama cha wauguzi James Maina alisema wauguzi wote 455 wa kaunti hiyo wamegoma kazi.Nakuru, Bomet, Kericho, Trans Nzoia, Uasin Gishu, Nandi, Elgeyo Marakwet na Turkana pia zimeathiriwa na mgomo huo.

Viongozi wa chama hicho pia wanataka wauguzi walioajiriwa chini ya mpango wa Afya kwa Wote (UHC) wapewe barua za ajira za kudumu na za pensheni, wakisema licha ya fedha kutengwa, wengi bado hawajapokea barua hizo.