Habari za Kitaifa

Matokeo ya KJSEA yatangazwa bila shamrashamra na kufungua enzi mpya Kenya

Na LINET IGADWAH December 12th, 2025 Kusoma ni dakika: 2

MATOKEO ya wanafunzi wa Gredi ya 9, KJSEA ndiyo yaliyokuwa ya kwanza jana kutolewa rasmi kupitia Mtaala wa Utendaji na Umilisi (CBE), tukio linaloonyesha jinsi mfumo wa elimu unavyoendelea kubadilika nchini.

Zamani kupitia mfumo wa 8-4-4 wanafunzi walitilia mkazo tu alama walizozipata ila mfumo huu unajikita sana katika talanta na uelewaji mpana wa masomo anayoyapenda mwanafunzi.

Chini ya mfumo wa CBE, mwanafunzi anatathminiwa kuanzia Gredi ya Kwanza hadi afanye KJSEA.

Chini ya uliokuwa mfumo wa 8-4-4, wanafunzi walikuwa wakifanya KCPE ambayo alama za mtahiniwa ndizo zilikuwa zikitathminiwa katika kila somo, alama ya jumla ikiwa 500.

Hata hivyo, KJSEA inachangia tu asilimia 60 ya alama ya mtahiniwa wa Gredi ya 9. Asilimia 40 zilizosalia nazo hugawanywa ambapo asilimia 20 hutoka kwa mtihani wa Gredi ya 6 KPSEA, kisha asilimia 20 nyingine huchangiwa na alivyofanya mwanafunzi katika masomo ya vitendo shuleni.

“Mfumo huu hautegemei alama katika mtihani mmoja tu bali maendeleo ya mwanafunzi kutoka madarasa ya chini,” akasema Afisa Mkuu wa Baraza la Kitaifa la Mtihani (KNEC) David Njengere.

“Mwanafunzi akiingia kwenye sekondari pevu, atakuwa akisomea masomo yanayoandamana na nguvu na talanta yake. Kwa hivyo, alama kwenye mtihani mmoja haitumiki kuamua matokeo yao,” akaongeza jana wakati wa kutangazwa kwa matokeo ya KJSEA jijini Nairobi.

Wanafunzi wa Gredi ya 9 hufanya masomo tisa huku kila somo likiwa na jumla ya alama nane. Kwa hivyo, mwanafunzi ambaye amepita zaidi na kuzoa alama zote huwa na jumla ya alama 72.

Mbali na alama pia wanafunzi hutathminiwa kwa vigezo vya kutimiza matarajio kabisa, kutimiza matarajio kwa wastani, kukaribia kutimiza matarajio na kukosa kutimiza matarajio.

Mfumo huu wa elimu unalenga kuhakikisha kuwa kuna usawa kwenye mazingira ya masomo ambapo pia talanta na uwezo wa kila mwanafunzi hupewa kipaumbele.

Wanafunzi hasa hawazingatii ushindani wa alama katika kila somo jinsi ilivyokuwa katika enzi za KCPE.

Katika KCPE, chini ya mfumo wa 8-4-4 alama za jumla zilikuwa 500 na watahiniwa walifanya mtihani kwenye masomo ya Kiswahili, Hesabu, Kingereza, Sayansi na Elimu Jamii ambayo ilikuwa inahusisha pia somo la dini.

Jana, matokeo ya KJSEA pia yalitolewa bila furaha na shamrashamra ambazo zilikuwa zikiandamana na kutangazwa kwa matokeo ya KCPE.

Kila mara matokeo ya KCPE yalipokuwa yakitolewa, wanafunzi walikuwa wakisherehekea pamoja na walimu na wanafunzi huku umma ukimakinikia shule zinazoongoza na zile zilizofanya vibaya.