Mawakili watishia kushtaki Ruto na Mchapishaji wa Serikali kwa kuajiri IEBC bila idhini
MAWAKILI ambao wanawakilisha raia wawili wanaopinga uteuzi wa mwenyekiti na makamishina wa Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka Nchini (IEBC), sasa wanawazia kuchukua hatua za kisheria dhidi ya Rais William Ruto na Mchapishaji wa Serikali kwa kupuuza amri ya korti.
Wakiongozwa na Wakili Paul Muite, mawakili hao pia wanasema kuwa huenda pia wakamshtaki Mwanasheria Mkuu Dorcas Oduor na Spika wa Bunge la Kitaifa Moses WetangĂșla kwa kukiuka amri ya korti kuhusu teuzi hizo.
Msimamo wa mawakili hao unatokana na kile walichosema ni ukiukaji wa amri ya Mahakama Kuu ambayo ilizuia kuteuliwa, kuchapishwa kwenye gazeti rasmi la serikali au kuapishwa kwa watu saba ambao waliteuliwa mwezi uliopita kuhudumu kama makamishina wa IEBC.
Bw Muite alisema kuchapishwa kwa orodha ya walioteuliwa kwenye gazeti rasmi la serikali ni ukiukaji wa amri ya korti na ni kitendo haramu.
Waliowasilisha kesi dhidi ya makamishina hao wa IEBC ni Kelvin Roy Omondi na mwanaharakati Boniface Mwangi ambao walisema hatua ya Rais Ruto na kuchapishwa majina hayo kwenye orodha ya serikali, ni kudharau korti.
Saba ambao uteuzi wao umezua utata ni Erastus Edung Ethekon (Mwenyekiti), Makamishina Hassan Noor Hassan, Mary Karen Sorobit, Anne Nderitu, Moses Alutalala Mukwana, Francis Odhiambo Aduol na Fahim Araphat Abdallah.
Kwa sasa hatua yao ya mwisho kuchukua madarakani ni kuapishwa kwao, shughuli ambayo inastahili kuongozwa na Jaji Mkuu Martha Koome.
Amri hiyo ya korti ambayo ilizua utata ilitolewa na Jaji Lawrence Mugambi mnamo Mei 29, 2025 baada ya kusikizwa kwa ombi la wawasilishaji wa kesi lililotaka amri itolewe kuzuia uteuzi huo.
Kwa kina, amri hiyo ilizuia kuchapishwa, kuapishwa au kuchukua afisi kwa watu hao saba hadi kesi hiyo isikizwe na iamuliwe.
Wiki iliyopita, pande zote zilifika mbele ya majaji watatu Roseline Aburili, John Chigiti na Bahati Mwamuye ambao amri hiyo iliyowekwa awali haikuondolewa.
Majaji hao walisema tu kesi hiyo itasikizwa mnamo Juni 23.
Bw Muite alisema amri hiyo ilitolewa baada ya kusikizwa kwa pande zote na kwa kuwa sasa hawaridhishwa na hatua aliyochukua Rais Ruto, wana haki ya kuwasilisha rufaa.
Kwenye uamuzi wake wa awali, Jaji Mugambi alisema waliowasilisha kesi walikuwa wametimiza vigezo vyote vya kupata amri kuzuia uteuzi wa makamishina na mwenyekiti wa IEBC.
Mabwa Omondi na Mwangi kwenye kesi yao wanadai Rais alikiuka katiba kwa kukosa kuzingatia usawa wa kieneo na kukosa kushauriana na upinzani au muungano wa upinzani jinsi inavyotakikana kisheria.
Pia walisema jopo la uteuzi halikuweka wazi ripoti yake au alama ambazo kila aliyehojiwa alipata. Aidha wanadai kuwa Mabw Ethekon, Hassan na Bi Sorobit na Bi Nderitu hawakufaa kuteuliwa kwa sababu wameonyesha miegemeo ya wazi ya kisiasa na hakuna uwazi wowote ambao wameuonyesha.