Mbarire awakia Kindiki kwa kuzuru Embu bila kumhusisha
GAVANA wa Embu Cecily Mbarire amelalamikia kudharauliwa na baadhi ya viongozi wa serikali kuu huku akionekana kumlenga Naibu Rais Profesa Kithure Kindiki ambaye alihudhuria mikutano mjini Embu wiki jana bila kumhusisha.
Mnamo Ijumaa, Profesa Kindiki alifanya ziara ya kushtukiza mjini Embu ambako alizungumzia utovu wa usalama ambao umekuwa ukiongezeka mjini na viungani mwa Embu.
Duru zinaarifu kuwa Bi Mbarire hakufahamu kuhusu ziara ya Profesa Kindiki na alihisi kuwa alitengwa, ubabe wa siasa za eneo hilo ukitajwa.
Gavana huyo amekuwa akishughulishwa katika mipango na ziara ya maafisa wa serikali ya kitaifa na mnamo Ijumaa hata viongozi wa kaunti walisema hawakufahamishwa kuhusu ziara ya Profesa Kindiki.
“Kuna baadhi ya viongozi ambao wanahudumu serikalini na wanafanya mikutano usiku Embu ili kupanga siasa za Embu bila kunihusisha au viongozi waliochaguliwa,” akasema Bi Mbarire wakati wa maadhimisho ya Sikukuu ya Madaraka.
“Naelewa siasa za nchi na sitakubali mtu yeyote bila kujali wadhifa anaoshikilia serikali kunitatiza au kupuuza uongozi wangu. Kupanga mikutano ya kisiasa bila kuhusisha viongozi waliochaguliwa ni utovu wa heshima,” akaongeza gavana huyo akionekana kumlenga Profesa Kindiki.
Wakati wa ziara ya Ijumaa ni Seneta Alexander Mundigi pekee aliandamana na Profesa Kindiki na hata hakupewa nafasi ya kuhutubia wananchi mjini humo.
Mkesha wa ziara hiyo, wandani wa Bi Mbarire walipuuza taarifa kuwa naibu rais alikuwa azuru eneo hilo wakisema zilikuwa porojo.
Kauli ya Bi Mbarire imeibua mgawanyiko mkubwa ambao unaendelea kutokota Mlima Kenya Mashariki ndani ya Kenya Kwanza.
Hapo awali, Rais Ruto au naibu wake walipozuru Embu, Bi Mbarire amekuwa mstari wa mbele kutoa wito kwa raia wajitokeze kuwalaki.
Pia gavana huyo hakufika kuhudhuria ibada ya maombi ya kila mwaka Jumatano iliyopita katika hoteli ya Safari Park Nairobi.
Kando na kuwa gavana, Bi Mbarire ndiye mwenyekiti wa UDA huku Profesa Kindiki akiwa naibu kiongozi wa chama.
Kuendeleza maasi dhidi ya serikali, Bi Mbarire alisema anapinga mswada unaolenga kuondoa Muguka kati ya mimea inayotambuliwa.
Alisema mswada huo unaodhaminiwa na Mbunge wa Kilifi Owen Baya unalenga kuondoa muguka kwenye orodha hiyo ilhali ndiyo tegemeo kiuchumi kwa wakazi wa Embu.
Mauzo ya muguka unachangia Sh22 bilioni kwa uchumi wa Kaunti ya Embu na Bi Mbarire alisema hatamruhusu yeyote kusambaratisha uchumi wa watu wa Embu.