Mbwembwe zatawala Madaraka Dei, huko Kilifi Aisha Jumwa akikanywa asitatize Mung’aro
WITO wa amani, ushirikiano na utulivu wa kisiasa Jumapili ulitanda maeneo mbalimbali huku baadhi ya magavana wakisusia sherehe na vijana wakizua vurugu wakati wa maadhimisho ya Sikukuu ya Madaraka Dei.
Sherehe za kitaifa ziliandaliwa uga wa Raila Odinga Kaunti ya Homa Bay huku kaunti mbalimbali zikiandaa Madaraka Dei maeneo yao, matukio mseto yakishuhudiwa.
Katika Kaunti ya Kisii baadhi ya vijana walitatiza kwa muda usomaji wa hotuba ya Rais William Ruto kwenye uwanja wa Gusii.
Sherehe hizo zilijaa mbwembwe na madoido tangu zilipoanza lakini ilipotimia zamu ya Kamishina wa kaunti ya Kisii Joseph Kibet kuisoma hotuba ya rais, vijana hao walianza kupiga kelele na kumzomea.
Vijana hao walikuwa wameketi katika jukwaa la G6, ambalo ni maarufu sana kwa visa vya uhuni ugani humo. Wakirukaruka na kurusha chupa za maji hewani, vijana hao walitoa kauli za “Ruto Must Go” (Ruto Lazima Aende) huku wengine wakitoa kibwagizo cha “One Term” (Muhula Mmoja).
Gavana wa Kisii Simba Arati alipoona kelele hizo zinakolea, aliingilia kati na kuuliza vijana hao wamruhusu kamishina akamilishe usomaji wa hotuba ndefu ya rais.
“Tafadhali vijana, ruhusuni kamishina wa kaunti atamatishe kusoma hotuba ya rais,” akasema Bw Arati huku vijana hao wakioenakana kutotetereka na kuendelea na kelele zao.
Katika Kaunti ya Trans Nzoia Gavana George Natembeya alisusia sherehe hizo katika Shule ya Msingi ya Bidii huku Waziri wa Afya wa Kaunti Sam Ojwang akiongoza sherehe hizo ambapo Kamishina wa Kaunti ya Trans Nzoia George Oyagi pia alikwepo.
Kwenye Kaunti ya Kilifi viongozi walitumia sherehe zilizoandaliwa eneobunge la Ganze kuwakashifu wapinzani wa Gavana Gideon Mung’aro ambao wameanza kampeni za mapema.
“Fanyeni kazi na gavana kwa sasa kisha 2027 ikifika mchape siasa badala ya kuwagawanya watu wetu,” akasema Mbunge wa Kaloleni Paul Katana kwenye hafla hiyo.
Kauli hiyo ilionekana kumlenga aliyekuwa Waziri wa Jinsia Aisha Jumwa ambaye analenga ugavana mnamo 2027 na ni mpinzani mkuu wa Bw Mung’aro.
Kwenye Kaunti ya Lamu Gavana Issa Timamy aliwaomba vijana wamheshimu Rais Ruto. Alikuwa akihutubu Shule ya Msingi ya Hindi Lamu Magharibi ambapo pia alishutumu upinzani ukiongozwa na aliyekuwa Naibu Rais Rigathi Gachagua kwa kueneza siasa za mgawanyiko.
“Vijana wana haki ya kukosoa serikali lakini wafanye hivyo kwa kutumia hekima na heshima wakifuata sheria,” akasema Bw Timamy.
Kamishina wa Kaunti ya Lamu Wesley Koech alitaja umuhimu wa ushirikiano kati ya washikadau wote kuhakisha usalama eneo hilo.
Kwenye Kaunti ya Mombasa Mbunge wa Likoni Mishi Mboko alisema kuwa ni umoja ndio utahakikisha taifa linastawi kimaendeleo. Sherehe hizo ziliandaliwa uwanja wa Mbuzi eneobunge la Nyali.
Kaskazini mwa Kenya, Gavana Nathif Jama aliongoza sherehe za Madaraka katika eneo la Modogashe ambapo aliahidi kuwa zaidi ya nyumba 150 sasa zitaunganishiwa maji kwa mara ya kwanza tangu uhuru.
Sherehe za Madaraka Kaunti ya Kakamega ziliandaliwa katika Shule ya Msingi ya Malava na kuongozwa na Gavana Fernandes Barasa ambaye aliwaomba viongozi wa kaunti hiyo waungane naye kutimiza ahadi zake.
Taarifa za Valentine Obara, Kalume Kazungu, Wycliffe Nyaberi, Manase Otsialo, Evans Jaola