Mdhibiti bajeti alivyokataa maombi ya Mbadi ya kutoa Sh72 bilioni
MIPANGO ya Wizara ya Fedha katika mwaka wa kifedha uliomalizika Juni 2026 ilikumbwa na kizingiti kikubwa, baada ya Mdhibiti wa Bajeti, Margaret Nyakang’o, kuzuia matumizi ya Sh72 bilioni.
Hiki ndicho kiasi kikubwa zaidi ambacho ofisi yake imewahi kuzuia katika miaka ya hivi punde.
Dkt Nyakang’o, ambaye Katiba imempa jukumu la kusimamia matumizi ya fedha za umma, alikataa maombi ya kutolewa kwa fedha hizo.
Hatua hiyo ilimzuia Waziri wa Fedha, John Mbadi kutoa idhini ya matumizi ya fedha kwa baadhi ya taasisi za serikali ambazo hutumia mabilioni kuendesha shughuli zao.
Fedha hizo ziliombwa chini ya Kifungu cha 223 cha Katiba, kinachoruhusu serikali kutumia fedha bila idhini ya kawaida ya Bunge katika hali maalumu.
Utaratibu huo hutumika pale ambapo fedha zilizotengewa shughuli fulani hazitoshi au wakati wa dharura kama majanga.
Hata hivyo, matumizi hayo lazima yaripotiwe Bungeni ndani ya miezi miwili.
Tangu Julai 2022, Wizara ya Fedha imeidhinisha taasisi za serikali kutumia Sh523 bilioni chini ya Kifungu cha 223. Kati ya kiasi hicho, Ofisi ya Mdhibiti wa Bajeti imekataa matumizi ya Sh158.6 bilioni.
Ofisi hiyo sasa inapendekeza sheria zinazodhibiti matumizi ya kifungu hicho zipitiwe upya ili kuimarisha usimamizi wa fedha za umma na kulinda uaminifu wa bajeti.
Dkt Nyakang’o amekuwa akionya dhidi ya matumizi mabaya ya kifungu hicho kukwepa idhini ya Bunge.
Miongoni mwa taasisi zilizozimiwa matumizi ya mabilioni ni Ofisi ya Rais, inayojumuisha Ikulu pamoja na ofisi za Rais, Naibu Rais na Mkuu wa Mawaziri.
Dkt Nyakang’o alikataa maombi ya kutolewa kwa Sh7.8 bilioni ambazo wizara ya fedha ilikuwa tayari imeidhinisha.
Katika mwaka wa kifedha wa 2025/26, wizara hiyo iliidhinisha ofisi hizo kutumia Sh12.9 bilioni chini ya Kifungu cha 223.
Hata hivyo, Mdhibiti wa Bajeti aliidhinisha Sh5.1 bilioni pekee, sawa na asilimia 39 ya fedha zilizoombwa.
Ripoti hiyo inasema baadhi ya maombi yalihusu shughuli za kawaida za kila siku ambazo zingetarajiwa wakati wa kuandaa bajeti.
“Matumizi chini ya Kifungu cha 223 yanapaswa kufanywa kwa kuzingatia masharti yake,” Dkt Nyakang’o alisema.
Kwa mwaka uliomalizika Juni 2026, wizara ya fedha iliidhinisha Sh281.5 bilioni kutolewa chini ya kifungu hicho kwa taasisi mbalimbali za serikali.
Lakini Mdhibiti wa Bajeti aliidhinisha Sh209.4 bilioni pekee.
Hii ina maana kuwa maombi ya kutumia Sh72 bilioni yalikataliwa.
Ikulu ilizimiwa Sh7.3 bilioni.
Kati ya Agosti 9, 2025 na Aprili 6, 2026, Waziri Mbadi alitoa idhini sita za Ikulu kutumia Sh11.8 bilioni kwa kile kilichoelezwa kuwa “gharama nyingine za uendeshaji”.
Hata hivyo, Mdhibiti wa Bajeti aliidhinisha Sh4.45 bilioni pekee na kukataa maombi manne yenye thamani ya Sh7.3 bilioni.
Miongoni mwa maombi yaliyokataliwa ni Sh5 bilioni yaliyoidhinishwa Desemba 12, 2025, Sh1 bilioni ya Aprili 6, 2026 na maombi mawili ya Sh800 milioni kila moja.
Ofisi ya Naibu Rais Kithure Kindiki pia ilizuiwa kutumia Sh418.7 milioni, ambazo kwa kiasi kikubwa zilikusudiwa kugharamia ukarimu na ukodishaji wa magari.
Wizara ya Fedha iliidhinisha ofisi hiyo kutumia Sh1.05 bilioni chini ya Kifungu cha 223.
Lakini Mdhibiti wa Bajeti aliidhinisha Sh245.5 milioni pekee kutoka kwa moja ya maombi hayo.
Ofisi ya Mkuu wa Mawaziri Musalia Mudavadi pia ilizuiwa kutumia Sh80 milioni ambazo wizara ya fedha ilikuwa imeidhinisha.
Ripoti hiyo inaonyesha kuwa ofisi zilizo chini ya urais zilitumia jumla ya Sh33 bilioni katika mwaka huo.
Fedha nyingi zilitumika katika shughuli za kawaida kama mishahara, kuandaa hafla na safari za maafisa wakuu wa serikali.