Habari za Kitaifa

Mjane wa Ng’eno asalimu amri, ajiondoa kinyang’anyiro cha Emurua Dikirr

Na VITALIS KIMUTAI March 24th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

KAMPENI za kuwania mchujo wa UDA katika eneobunge la Emurua Dikirr zimefikia kipindi cha lala salama huku ikibainika wazi kuwa mjane wa marehemu mbunge Johana Ng’eno, amejiondoa kinyang’anyironi.

Naiyanoi Ng’eno alijiondoa kwenye mapambano ya kisiasa ya kumrithi mumewe kutokana na sababu za kibinafsi baada ya kushauriana na familia yake.

Bi Naiyanoi alikuwa ameidhinishwa na familia yake majuma mawili yaliyopita na alikuwa akionekana kuwa kifua mbele kutwaa kiti hicho.

Kujiondoa kwake kumepisha kampeni kali miongoni mwa wandani wa Bw Ng’eno ambao wanasaka kiti hicho.

“Naiyanoi hatakuwa akigombea kiti hicho cha ubunge, amekuwa akiugua na bado ameathirika sana kwa kumpoteza mumewe. Kutokana na hilo kama familia yake tumeamua tumwepushe na kampeni kali ambazo zinatarajiwa,” akasema Bw Ngetich.

Bi Naiyanoi hakujibu maswali kuhusu mwelekeo ambao atauchukua huku familia yake ikithibitisha uamuzi huo uliafikiwa Alhamisi wiki iliyopita.

Mnamo Jumamosi, wandani wa marehemu Bw Ng’eno waliungana na kumuidhinisha Benard Ng’eno, msaidizi wa kibinafsi wa marehemu kama mgombeaji wanayemuunga mkono.

Bw Ng’eno sasa atapambana na mfanyabiashara David Keter, Afisa wa Polisi Kibet Rotich na Mhasibu Joseph Kiprono Koech.

Haya yalitokea huku UDA ikisema uteuzi wa chama utakuwa huru na haki.

Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka Nchini (IEBC) nayo imetoa Mei 14 kama tarehe ya kufanyika kwa uchaguzi mdogo.

Emurua Dikirr inawapiga kura 44,447 na vituo 94 vya kupiga kura huku uchaguzi wenye mdogo ukitarajiwa kugharimia Sh59 milioni.

Wakati huo huo, Diwani wa Wadi ya Elkerin Ezekiel Korir, ametangaza kuwa atamuunga mkono mfanyabiashara David Keter.

Bw Keter alikuwa ameshindwa na Bw Ng’eno kwenye chaguzi mbili zilizopita na ameeleza imani kuwa atashinda kiti hicho.

“Nina wingu la matumaini kuwa wakazi wa Emurua Dikirr watanichagua ili nikamilishe miradi ya maendeleo ambayo ilianzishwa na pia nianzishe miradi mipya,” akasema Bw Keter.