Habari za Kitaifa

Mkakati maalum wa kushughulikia maandamano ya wiki ijayo wakamilishwa

Na KAMORE MAINA June 20th, 2025 Kusoma ni dakika: 2

MAAFISA wakuu wa polisi walikutana jijini Nairobi Alhamisi kukamilisha mikakati ya kushughulikia maandamano yanayopangwa kuanza wiki ijayo na yanayotarajiwa kudumu kwa siku kadhaa.

Katika kikao hicho, walikabidhi Baraza la Kitaifa la Usalama (NSC) mkakati huo katika mkutano uliohudhuriwa na Rais William Ruto. Mkakati huo unaeleza jinsi polisi wanavyonuia kushughulikia maandamano hayo huku wakidumisha amani, hasa jijini Nairobi.

Mazungumzo ya awali yalifanyika Jumanne katika makao makuu ya Huduma ya Kitaifa ya Polisi (NPS) katika Jogoo House. Kikao cha pili kilifanyika Jumatano ambapo mkakati wa pamoja wa operesheni uliandaliwa na kukubaliwa kabla ya kuwasilishwa kwa NSC.

Miongoni mwa waliohudhuria mkutano huo ni Inspekta Jenerali wa Polisi Douglas Kanja, Mkurugenzi wa Idara ya Upelelezi wa Jinai (DCI) Mohammed Amin, Naibu Inspekta Jenerali wa Polisi Gilbert Masengeli, na kaimu Naibu Inspekta Jenerali Patrick Tito.

Kwa mujibu wa vyanzo vya usalama, Kanja anaongoza maandalizi hayo. Akizungumza na Taifa Leo Alhamisi jioni, alisisitiza kuwa polisi wako tayari kuhakikisha kuna utulivu huku wakiheshimu haki ya wananchi kuandamana kwa amani.

“Ndio, tuko tayari. Leo tumekutana na makamanda wote kupitia upya mkakati wetu wa usalama. Polisi watafuata taratibu zote zilizowekwa, na ninawaomba waandamanaji wawe na amani na wazingatie maagizo ya polisi,” alisema Kanja.

Alisisitiza: “Yeyote mwenye nia ya kuvuruga maandamano kwa ghasia, ajiandae kuishi muda mrefu gerezani.”

Vyanzo vya usalama vimebaini kuwa Jumatatu, saa chache baada ya Naibu Inspekta Jenerali wa Polisi Eliud Lagat kutangaza kujiondoa kwa muda ili kupisha uchunguzi kuhusu kifo cha mwalimu na mwanablogu Albert Ojwang, Kanja na Waziri wa Usalama wa Ndani Kipchumba Murkomen walihudhuria mkutano katika Ikulu. Kikao hicho kililenga kuandaa mikakati mahsusi ya kushughulikia maandamano hayo, hasa jijini Nairobi.

Kama sehemu ya maandalizi, mamia ya maafisa wa polisi watatumwa katikati ya jiji la Nairobi na maeneo mengine muhimu kuanzia Jumatano, Juni 25, siku ambayo maandamano yanatarajiwa kuanza.

Maafisa kutoka vitengo mbalimbali wakiwemo wa Kitengo cha Kukabiliana na Fujo (GSU), Kitengo cha kukabiliana na dharura (RDU), na kitengo polisi wa kawaida watakuwa mitaani kufuatilia hali.

Watakaopiga doria kwa miguu watasaidiwa na wenzao kwenye magari ya doria na malori, ili kuhakikisha wanajibu haraka endapo hali itazidi.

GSU na polisi wa Utawala watahusika moja kwa moja katika kuvunja maandamano yatakayogeuka ghasia.

Kwa maandamano ya amani, kikosi maalum kutoka Kituo cha Polisi cha Nairobi Central wamepewa jukumu la kulinda waandamanaji. Hii ni kwa matarajio kwamba maandamano yatakuwa yenye utulivu na nidhamu.

Mpango wa polisi pia unahusisha matumizi ya magari ya kurusha maji ya mwasho kuwatawanya waandamanaji yatakayowekwa katika maeneo muhimu.

Vile vile, magari ya polisi na malori yatatumika kufunga barabara zinazoelekea maeneo muhimu kama Bunge, Ikulu, na majengo mengine ya serikali. Baadhi ya barabara zitafungwa na taarifa kuhusu njia mbadala zitatolewa mapema.

Kwa kutegemea jinsi hali itakavyokuwa wakati wa maandamano, polisi wanaweza pia kuwatumia maafisa waliopanda farasi na kikosi cha mbwa ili kuimarisha  usalama.

Tofauti na maandamano ya Juni 2024 ambapo polisi walidaiwa kutojipanga, wakati huu makamanda wa polisi wa vituo wameagizwa kukusanya taarifa za kijasusi mapema. Maafisa kutoka Idara ya Ujasusi wa Kitaifa (NIS) wamepewa jukumu la kuwatambua waandalizi na wafadhili wa maandamano.

Ili kurahisisha mawasiliano wakati wa maandamano, maafisa wakuu wa polisi watakuwa katika Kituo Kikuu cha Usimamizi wa Polisi kilichoko Jogoo House ambapo watasimamia na kutoa mwongozo kwa vikosi barabarani.

Msemaji wa Huduma ya Kitaifa ya Polisi Michael Muchiri alithibitisha kuwa mikutano ya kupanga kukabili maandamano inaendelea kila mara: “Ni mkutano baada ya mkutano. Tunataka kuwa tayari kikamilifu na tutatoa usalama wa kutosha,” alisema.

Kamanda wa Polisi eneo la Nairobi, George Seda, aliwahakikishia wakazi wa jiji kwamba usalama wa kutosha umewekwa: “Tutatoa usalama kwa waandamanaji na kwa Wakenya wengine wote,” alisema Jumatano katika mkutano na wanahabari ofisini kwake.