Mkenya Steve Munyakho aliyeponea kunyongwa Saudi Arabia kurejea nyumbani baada ya Ramadhani
BARAZA la Waislamu Nchini (SUPKEM) limethibitisha kuwa fidia ya Sh129.5 milioni ya kuwezesha kuachiliwa huru kwa Mkenya, Stephen Munyakho, aliyehukumiwa kunyongwa Saudi Arabia, zimelipwa.
Kwenye kikao na wanahabari Ijumaa (Machi 28, 2025) jijini Nairobi mwenyekiti wa baraza hilo Hassan Ole Naado alisema kuwa taratibu za kumwachilia huru zitaanza wiki hii baada ya kukamilika kwa Mwezi Mtukufu wa Ramadhan.
“Kama kawaida wakati kama huu wa Ramadhan, mahakama nchini Saudi Arabia hazifanyikazi. Kwa kuwa mwezi huu Mtukufu unaelekea kuisha, ninaamini kuwa Mahakama itaanza kutayarisha kibali cha kuachilia mwenzetu wiki ijayo (wiki hii),” akaeleza.
Ole Naado alisema pesa hizo zilitolewa na Baraza la Waislamu Ulimwenguni (Muslim World League-MWL) zilikabidhiwa kwa familia ya mwanamume ambaye alikufa 2012 baada ya kupigana na Bw Munyakho nchini Saudi Arabia.
“Baraza la Waislamu Ulimwenguni lilitoa pesa hizo mwezi jana kufuatia juhudi zilizoendeshwa na SUPKEM pamoja na washirika wegine. Hii ni baada ya mama Steve kutembelea afisi zetu mwaka jana kuomba usaidizi. Tulilivalia njuga suala hilo na kuanzisha mazungumzo na washirika kadhaa nchini Saudi Arabia,” mwenyekiti huyo akaeleza.
Suala hilo lilipewa kipaumbele baada ya uongozi wa SUPKEM kufanya mkutano na viongozi wa Baraza la Waislamu Ulimwenguni kukutana Nairobi mnamo Agosti 13, 2024.

Wakati wa mkutano huo Katibu Mkuu wa MWL Dkt Mohamed AbdulKarim Alissa, alijulishwa kuhusu kesi ya Munyakho na kuombwa aingilie kati.
Kulingana na Ole Naado, kwa kuwa Munyakho na marehemu walikuwa marafiki kabla ya wao kupigana, suala hilo lilichukuliwa kwa uzito katika baraza la MWL.
Mamake Munyakho, Dorothy Kweyu, aliongea na wanahabari kupitia mtandao wa WhatsApp na kuthibitisha kuwa Sh129.5 milioni zilizotolewa na baraza la MWL zimelipwa familia ya mhasiriwa.
“Mimi kama mamake Stevo nathibitisha kuwa Baraza la Waislamu Ulimwenguni limelipa pesa za fidia ya damu kwa familia ya marehemu aliyekufa kwa bahati mbaya baada ya kupigana na mwanangu wakiwa kazini Saudi Arabia. Sasa tunasubiri mahakama kuandaa kibali cha kuachiliwa huru kwa Stevo kutoka gerezani ili arejee nyumba,” akaeleza.
Mama Kweyu, ambaye ni mwanahabari tajika, alitoa shukrani kubwa kwa baraza la MWL na wahisani wote waliojitokeza kutoa michango ya kusaidia kulipa fidia hiyo.
“Ama kwa hakika natoa shukrani kubwa zaidi kwa usaidizi huo. Tulikuwa tumefaulu kuchanga Sh20 milioni pekee ambazo zilikuwa kiasi kidogo zaidi zikilinganishwa na Sh129.5 milioni zilizotakikana. Aidha, nashukuru vyombo vya habari kwa kusaidia kuendesha michango na kuangazia madhila ya mtoto wangu Stevo,” akaeleza.
Habari kuhusu kulipwa kwa fidia hiyo ilifichuliwa kwa mara ya kwanza na Katibu Mkuu wa chama cha United Democratic Alliance (UDA) Hassan Omar Jumanne wakati wa Iftar iliyoandaliwa katika Ikulu ya Nairobi.