Mmiliki mpya wa NMG aahidi kutunza hadhi
MMILIKI mpya mkuu wa Nation Media Group (NMG), mfanyabiashara Rostam Azizi, ameahidi kudumisha viwango vya uandishi wa habari na utamaduni wa uhariri uliosaidia kujenga imani ya umma kwa mojawapo ya kampuni kubwa za vyombo vya habari barani Afrika kwa zaidi ya miaka 66.
Mwekezaji huyo kutoka Tanzania, kupitia kampuni yake ya Taarifa Ltd, anatarajiwa kununua asilimia 54.08 ya hisa za NMG kutoka kwa shirika la Aga Khan Fund for Economic Development (AKFED).
Muamala huo unatarajiwa kukamilika ndani ya miezi mitatu hadi minne ijayo baada ya kupata idhini ya mashirika ya udhibiti.
AKFED inamiliki hisa hizo kupitia kampuni ya uwekezaji inayojulikana kama NPRT Holdings Africa Limited, ambayo sasa itahamishiwa Taifa Group.
Akizungumza na wanahabari Machi 11, 2026, Bw Azizi alisema NMG imekuwa na nafasi muhimu katika kukuza sekta ya habari Afrika Mashariki katika kipindi cha zaidi ya miongo sita chini ya uongozi wa Aga Khan IV na AKFED.
Aliongeza kuwa ushirikiano huo mpya utaendeleza urithi huo huku ukiweka msingi wa ubunifu na ushirikiano zaidi wa kikanda.
Alisisitiza kuwa vyombo vya habari vilivyo huru na vinavyoaminika vina mchango mkubwa katika kuimarisha ushirikiano wa Afrika Mashariki pamoja na kuboresha utawala bora na viwango vya kitaaluma.
“NMG kwa miongo kadhaa imekuwa mstari wa mbele katika kuunda mijadala ya umma kote Afrika Mashariki na kuimarisha uhusiano kati ya watu wa eneo letu. Kupitia uwekezaji huu nitaungana na kampuni kama mshirika wa kimkakati wa muda mrefu kusaidia ukuaji, ubunifu na mageuzi yake katika enzi hii ya kidijitali,” alisema Bw Azizi.
Aliongeza kuwa uwekezaji huo ni ishara ya kuunga mkono mustakabali wa uandishi wa habari barani Afrika wakati ambapo teknolojia inaendelea kubadilisha namna taarifa zinavyozalishwa na kutumiwa katika sekta ya habari duniani.
Tangu kuanzishwa kwake mwaka wa 1959, NMG imestawi na kuwa shirika la vyombo vya habari lililo na majukwaa mengi, likihudumu katika nchi nne za Afrika Mashariki na kusimamia zaidi ya chapa 30 huku likiajiri zaidi ya wataalamu 1,000 katika eneo hilo.
Bw Azizi ni mwekezaji mwenye uzoefu mkubwa katika biashara mbalimbali Afrika Mashariki.
Aliwahi kuwa mmoja wa waanzilishi na mwenyehisa wa Mwananchi Communications Ltd kati ya mwaka 2000 na 2006, kampuni iliyochapisha magazeti ya The Citizen, Mwananchi na Mwanaspoti, ambayo baadaye yalinunuliwa na NMG mwaka 2006.
AKFED ilisema kuondoka kwake katika uwekezaji NMG ni sehemu ya mkakati mpya wa kuzingatia sekta zake kuu kama huduma za kifedha, viwanda, miundombinu na ukarimu. NMG ilikuwa uwekezaji wake pekee katika sekta ya vyombo vya habari duniani.
Nation Media Group ilianzishwa na Aga Khan IV kwa maono ya kuipatia Kenya vyombo vya habari huru ili kusaidia kukuza utawala wa kidemokrasia wakati wa kuelekea uhuru.
Ilianza kama gazeti dogo la Kiswahili lililoitwa Taifa Leo, lililolenga kutoa sauti kwa Waafrika wengi katika miaka ya mwisho ya utawala wa kikoloni.