• Nairobi
  • Last Updated May 11th, 2024 7:15 PM
Mshukiwa ajaribu kujiua jela kwa kujikatakata na wembe

Mshukiwa ajaribu kujiua jela kwa kujikatakata na wembe

NA FARHIYA HUSSEIN

Mshukiwa aliyehusika katika jaribio la kufyatuliana risasi katika mahakama ya Mombasa inasemekana alijaribu kujitoa uhai akiwa seli.

Musa Salim anayekabiliwa na shtaka la wizi anasemekana kutumia wembe kujikata tumbo mara kadhaa katika gereza kuu la Shimo La Tewa.

Soma kisa kingine cha kujiumiza, mara hii kikihusu afisa wa polisi: Polisi ajiumiza mwenyewe kwa risasi mdomoni

Vyanzo vinavyochunguza tukio hilo hata hivyo vimefichua kuwa maafisa wanaosimamia gereza hilo waligundua majeraha kwa sababu ya damu kwenye nguo zake.

Tukio hilo limetokea siku moja tu baada ya kujaribu kunyakua bunduki kutoka kwa afisa wa magereza, na kutishia kuwapiga risasi wahudhuria vikao vya mahakama na hivyo kuzua hofu ndani ya chumba cha mahakama.

Majeraha hayo hayakuhatarisha maisha yake lakini ataendelea kufuatiliwa kabla ya kufikishwa mahakamani.

Kikao cha kawaida cha mahakama katika Mahakama ya Mombasa kilichukua mkondo wa kutatanisha Jumatano Januari 10, 2024 alasiri wakati mshtakiwa, alifika mbele ya hakimu mkuu alipotishia kuzua fujo kwa kunyakua bunduki kutoka kwa Afisa wa Magereza.

Kisa hiki ambacho hakijawahi kushuhudiwa kimeibua wasiwasi kuhusu itifaki za usalama ndani ya Mahakama ya Mombasa.

Wataalamu wa sheria, wafanyakazi wa mahakama, na wageni kwa pamoja wamesalia wakipambana na ukweli wa kushtua kwamba mahali palipokusudiwa kutoa haki kunaweza kuwa eneo la janga linaloweza kutokea.

Barua iliyoonekana na Taifa Leo iliyoelekezwa kwa Hakimu Mkuu wa Mahakama ya Mombasa ilisema “Tukio hilo lilitokea wakati mshtakiwa aliponyakua bunduki kutoka kwa Afisa wa Magereza na kujaribu kuwafyatulia risasi watu waliokuwa karibu lakini hakuweza kuifungua imimine risasi,” barua ilisomwa kwa sehemu.

Pia ilibainisha kuwa hata hivyo alizidiwa nguvu na maafisa waliokuwa wakishika doria katika mahakama hiyo na silaha ikachukuliwa kutoka kwake.

“Hakuna shaka kuwa hili ni tukio la kutisha na la kusikitisha ambalo halikupaswa kutokea. Ilibidi Hakimu Mfawidhi arudishwe kwenye vyumba vyake. Alishtuka baada ya tukio hilo na ilibidi mambo yote yaliyokuwa mbele yake yaondolewe.”

Mamlaka kutoka Kituo Kikuu cha Polisi waliarifiwa mara moja, na walibaini uchunguzi unaendelea ili kuelewa hali iliyosababisha uvunjifu huu wa kutisha wa usalama ndani ya mahakama.

  • Tags

You can share this post!

Kamwene: Makau Mutua amkinga Kalonzo dhidi ya makombora ya...

Masaibu ya Arati: ODM yataka hatua kali dhidi ya Osoro,...

T L