Mwanamume ashtakiwa kwa kutumia jina la binti ya Ruto kwenye kitabu
MWANDISHI mmoja Jumanne alifikishwa mbele ya mahakama ya Nairobi kwa tuhuma za kujitambulisha kama binti wa Rais William Ruto, Charlene Ruto, kwa kuchapisha kitabu chenye kichwa kilicho na jina lake.
Bw Webstar Ochora Elijah alishtakiwa kwa kosa la kujifanya binti ya rais kinyume na kifungu cha 382(1) cha Kanuni ya Adhabu.
Karatasi ya mashtaka ilieleza kuwa alichapisha kitabu kilichoitwa “Beyond the Name Charlene Ruto and the Youth Uprising”.
Inadaiwa kuwa alichapisha kitabu hicho kabla au kufikia Mei 22, 2025, kwa kushirikiana na wengine ambao bado hawajafikishwa mahakamani, kwa nia ya kudanganya.
Bw Ochora alikana mashtaka alipofikishwa mbele ya Hakimu Mkuu wa Milimani, Geoffrey Onsarigo.
Mahakama ilimwachilia kwa dhamana ya pesa taslimu Sh50,000. Kesi hiyo itatajwa Juni 17 kwa mwelekeo zaidi.
Mashtaka yanaeleza kuwa kitabu hicho kilitolewa bila idhini au taarifa kwa Charlene. Maafisa kutoka Idara ya Upelelezi wa Jinai (DCI) walimkamata Ochora Mei 30 na kumweka rumande katika Kituo cha Polisi cha Muthaiga.
Mahakama iliambiwa kuwa wataalamu wa uchunguzi wa kidijitali walikuwa wakichunguza laptopu yake na vifaa vingine vya kidijitali kwa ushahidi unaohusiana na uchapishaji huo.
Upande wa mashtaka pia ulisema kuwa Ochora anachunguzwa kwa kuvunja Sheria ya Matumizi Mabaya ya Kompyuta na Uhalifu wa Mtandaoni, kwa kutumia jina na picha ya Charlene bila idhini, katika njia isiyo sahihi na ya kupotosha.
Wakili wake, Evans Ondeki pamoja na wakili wa familia Kennedy Mong’are, walikosoa kukamatwa kwake wakisema ni ukiukaji wa haki za kikatiba, hasa uhuru wa kujieleza.
“Uhuru wa kujieleza unajumuisha haki ya kutumia watu mashuhuri katika maoni ya ubunifu,” alisema Ondeki, akiongeza kuwa kukamatwa kwa Ochora kunatuma ujumbe wa hofu kwa wabunifu wachanga nchini Kenya.
Mong’are alimtaja mshtakiwa kama mwandishi na mchapishaji anayeheshimika, aliyeandika kazi nyingine kuhusu viongozi wa kisiasa wa kimataifa kama Raila Odinga na aliyekuwa Rais wa Amerika Donald Trump.
“Alikuwa akifanya kazi ya kuandika kitabu kinachoonyesha picha nzuri ya Charlene Ruto,” Mong’are alieleza.
“Kumweka kizuizini bila kufuata utaratibu wa kisheria ni jambo la kusikitisha,” alisema.