Habari za Kitaifa

Ni siasa za mabavu serikali ikitumia nguvu kunyima Upinzani nafasi ya kutangamana

Na CECIL ODONGO, DAVID MUCHUI March 9th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

MATUKIO ya kisiasa yanayoendelea kushuhidiwa nchini yamezua hofu kuwa siasa za ukandamizaji na makabiliano zinarejea nchini kuelekea uchaguzi mkuu wa 2027.

Mnamo wikendi, Gavana wa Siaya James Orengo aliripoti kuwa walinzi wake walizuiwa kabla ya ziara ya Rais William Ruto katika Kaunti ya Siaya jana.

Jana, kulikuwa na makabiliano ambapo viongozi wa Upinzani walidaiwa kuzimwa na maafisa wa usalama kuhudhuria ibada katika Kanisa la Kimethodisti la Kaaga, Kaunti ya Meru.

Mitandaoni, Mbunge wa Embakasi Mashariki Babu Owino naye alilalama kuwa kuna mpango wa kumkamata, akihusisha afisa mmoja wa serikali na njama hizo.

Bw Orengo mnamo Jumamosi usiku alisema walinzi na wafanyakazi wanane wa kaunti walizuiliwa akihusisha tukio hilo na ziara ya Rais Ruto Siaya.

“Jioni hii (Jumamosi usiku) wafanyakazi wangu wamekamatwa na kuzuiliwa Siaya na Nairobi kuhusiana na ziara ya Rais eneo la Siaya,” akaandika Bw Orengo katika mitandao yake ya kijamii.

“Tabia hii ya polisi haina nafasi katika taifa ambalo msingi wake ni demokrasia. Ninataka waachiliwe huru,” akaongeza.

Gavana Orengo ni kati ya wanasiasa wanaoegemea mrengo wa Linda Mwananchi ambao wamekuwa wakipinga uongozi wa sasa wa ODM.

Amehudhuria mikutano ya vuguvugu hilo Kitengela, Busia na Amalemba katika Kaunti ya Kakamega.

Vuguvugu la Linda Mwananchi linajumuisha wabunge Babu Owino (Embakasi Mashariki), Caleb Amisi (Saboti), Seneta wa Vihiga Godfrey Osotsi na wanasiasa waasi wa ODM.

Bw Orengo pia amekuwa akipinga ushirikiano wa chama hicho na UDA huku akipinga vikali muafaka wa ushirikiano baina ya ODM na chama tawala.

Aidha, Bw Orengo wikendi alisema kuwa mrengo wake hautahudhuria Kongamano la Wajumbe (NDC) wa ODM ambalo linatarajiwa kufanyika Machi 27.

Viongozi wa upinzani walizuiwa kuhudhuria ibada ya Jumapili kanisani Kaaga Methodist ambapo pia Naibu Rais Prof Kithure Kindiki aliratibiwa kuhudhuria.

Viongozi hao walikuwa wamealikwa wahudhurie ibada ya kutawazwa kwa Askofu wa kanisa hilo David Mwiti Muthuiya.

Kulikuwa na maafisa wengi wa polisi nje ya kanisa hilo baada ya kubainika kuwa viongozi wa upinzani wangefika hapo.

Mkuu wa Mawasiliano wa Wiper Paloma Gatabaki alikuwa amewasili kuwatengea vinara hao viti nje ya hema ambalo Prof Kindiki alipangiwa kuketi.

Hata hivyo, muda mfupi baadaye, Paloma na wasaidizi wengine wa viongozi wa upinzani waliamriwa waondoke.

Bi Gatabaki alidai waliondolewa na polisi wa kupambana na ghasia.

“Tumefurushwa kanisani ingawa tulikuwa tumealikwa tuhudhurie. Polisi walituambia haturuhusiwi ndani,” akasema Bi Gatabaki.

Uongozi wa kanisa hilo, hata hivyo ulisema picha ya bango ambalo lililoonyesha viongozi wa upinzani wangehudhuria, ilikuwa feki.

Viongozi hao baadaye walihudhuria ibada katika Kanisa la Kipentekosti ambapo waliendelea kushambulia serikali na kusema watahakikisha Rais Ruto hachaguliwi tena 2027.

Bw Owino ambaye amekuwa mwiba kwa serikali alidai kulikuwa na mpango wa kumnyaka na makachero kutoka Idara ya Upelelezi Nchini (DCI).

Alichapisha stakabadhi ambapo alihusisha afisa mmoja wa serikali kama mlalamishi na kudai kuwa maafisa wanaotaka kumnyaka wanatoka Kaunti ya Kakamega.

“Huko kuandamwa hakunishughulishi. Serikali afadhali ifahamu mtu ambaye inapambana naye,” akaandika Bw Owino katika ukurasa wake wa Facebook.

Kiongozi wa ODM, Dkt Oburu Oginga, Mbunge wa Alego Usongo Samuel Atandi na wanasiasa wa ODM Nyanza wamekuwa mstari wa mbele kumkashifu Bw Orengo, baadhi ya nyakati wakimrejelea kama mwanasiasa mwasi.

Mchanganuzi wa masuala ya kisiasa Martin Andati anasema kuwa Rais Ruto anaiga tu makosa yaliyofanywa na mtangulizi wake Uhuru Kenyatta ilhali kitendo hicho kinawajenga tu wanasiasa wa Linda Mwananchi na upinzani.

“Anafuata tu vile Uhuru Kenyatta alikuwa akimfanyia na ukiangalia vitu vyote alivyokuwa akisema ni vibaya sasa anavifanya. Hata hivyo, kile anafanya kinawajenga kisiasa na watu watakuwa wakijazana katika mikutano yao,” akasema Bw Andati.

Hata hivyo, mchanganuzi huyo anasema viongozi hao wa upinzani nao pia lazima wajikakamue kwa sababu hawawezi kufikia hadhi ya marehemu Raila Odinga.

“Hawana jingine ila kuungana tu kwa sababu hicho ndicho kitawaokoa,” akaongeza.