Habari za Kitaifa

Nyama ya mamilioni ya pesa yakwama Kenya soko la Uarabuni likiharibiwa na vita

Na ANTHONY KITIMO, KALUME KAZUNGU March 12th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

WAUZAJI nyama nchini wanaouza bidhaa hiyo katika mataifa ya Uarabuni wanakadiria hasara baada ya soko hilo kuathirika na vita kati ya Israel na Iran.

Wafanyibiashara hao ambao wanakadiria hasara ya mabilioni ya pesa wanasema Mwezi Mtukufu wa Ramadhan huwa wakati ambapo soko la nyama linanawiri lakini kutokana na vita vinavyoendelea, tani nyingi za nyama zimekwama nchini.

Kufikia Jumatatu ya wiki hii, zaidi ya tani 300 za nyama zilikuwa zimekwama kwenye hifadhi humu nchini baada ya safari za ndege kusimamishwa na gharama za usafirishaji kuongezeka maradufu.

Mkurugenzi Mtendaji wa Wauzaji wa Nyama na Mifugo nchini (KEMLEIC), Bw Nicholus Ngahu, alisema sekta hiyo inapata hasara kubwa kwa sababu ya vita vinavyoendelea.

“Kati ya nyama yoyote tuliyochinja karibu wiki mbili zilizopita, ni sehemu ndogo tu iliyoweza kusafirishwa nje ya nchi. Tunakabiliwa na hasara kubwa kwani maghala ya baridi yanaanza kujaa kupita kiasi,” alisema.

Wiki iliyopita, Bw Ngahu alisema kuwa katika kipindi cha siku mbili tu walipata hasara ya zaidi ya Sh1 bilioni baada ya bidhaa hiyo kukosa kusafirishwa nje ya nchi.

Vita hivyo vinaendelea pia kuthiri soko la mauzo ya bidhaa nyingine kama vile parachichi, kahawa na chai.

Wauzaji wa bidhaa hizo ambao hutegemea usafirishaji wa baharini wamekumbwa na usumbufu katika biashara zao, huku bidhaa zinazoharibika haraka zikiwa katika hatari ya kupoteza ubora.

Mkurugenzi Mtendaji wa Baraza la Wamiliki wa Mizigo Afrika Mashariki (SCEA), Bw Agayo Ogambi, alisema kwa sababu meli zinachukua muda mrefu kufika Bandari ya Mombasa kutokana na kubadilishwa kwa njia za usafirishaji ili kuepuka njia za Bahari ya Shamu, muda wa kusafirisha bidhaa nje umeongezeka kwa siku 10 hadi 20 au zaidi.

“Tunakaribia kuanza kipindi cha kusafirisha parachichi nje ya nchi katika siku chache zijazo. Kuchelewa kwa usafirishaji, kutafanya parachichi nyingi zilizovunwa kupoteza ubora,” alisema Bw Ogambi.

Kwingineko, vita hivyo vimepelekea bandari ya Lamu kuandikisha historia kwa kupokea meli ya mzigo wa magari kwa mara ya kwanza tangu kuzinduliwa kwake miaka sita iliyopita.

Jumanne, meli iliyokuwa na shehena ya magari 1,200 iliwasili na kutia nanga Bandarini Lamu.

Meli hiyo kwa jina MV Grande Auckland ilikuwa inatoka Bara Uropa kuelekea Mashariki ya Kati kushukisha magari hayo.

Kufuatia misukosuko iliyochacha Mashariki ya Kati, meli hiyo ilielekezwa katika Bandari ya Lamu, ambapo ilishukisha magari 469 kati ya 1,200 huku yaliyosalia yakielekezwa maeneo mengine, ikiwemo Mumbai, India.

“Kutokana na misukosuko ya Mashariki ya Kati, mzigo huu utasalia chini ya ulinzi wetu kwa muda,” akasema Meneja Mkuu wa Bandari ya Lamu, Bw Abdulaziz Mzee.

Kwa upande wake, Meneja Msimamizi wa Kampuni ya Uchukuzi wa Meli ya Nisomar Afrika, Bw Munir Minas Hussein, alisema walichukua hatua hiyi kwa sababu za kiusalama, hasa kuhusu yale yanayoendelea kwenye Bahari ya Shamu na Mashariki ya Kati kwa jumla.