Nyoro ni fuko wa Serikali? Wakosoaji wadai chama chake ni mkakati wa kuvuruga Upinzani
RAIS William Ruto aliwahi kumtaja Mbunge wa Kiharu, Ndindi Nyoro, kama mwanasiasa chipukizi ambaye angepewa malezi kuwania uongozi wa kitaifa.
Katika mahojiano ya pamoja na wanahabari yaliyofanyika Sagana State Lodge mnamo Machi 31, 2025, Rais Ruto alimtaja Nyoro kama “kiongozi mzuri sana” na kufichua kuwa alikuwa akimlea kisiasa.
“Ni kijana ninayemlea kisiasa. Kuna mambo siwezi kuyasema hapa. Ndindi Nyoro ni kiongozi na ni mmoja wa vijana ninaowakweza kisiasa,” alisema Rais Ruto wakati huo.
Hata hivyo, chini ya miezi 18 baadaye, uhusiano huo wa kisiasa unaonekana kufikia kikomo baada ya Nyoro kujitenga rasmi na chama tawala cha United Democratic Alliance (UDA) na kutangaza kujiunga na upinzani.
Mnamo Jumatatu usiku, mbunge huyo wa Kiharu alizindua rasmi chama kipya kiitwacho Peoples’ Party of Kenya (PPK) katika Hoteli ya Safari Park, Nairobi, na kutangaza kwamba, sasa atashirikiana na viongozi wa upinzani kutafuta mwelekeo mpya wa kisiasa na kiuchumi kwa Kenya.
Tangazo hilo lilimaliza miezi ya uvumi kuhusu hatima yake kisiasa, lakini pia likaibua maswali makubwa kuhusu nia yake halisi ya kisiasa.
Je, Nyoro anajenga vuguvugu huru la kisiasa lenye mtazamo wa kitaifa?
Je, anajiandaa kuwania urais mwaka 2027? Au chama chake kipya ni sehemu ya mkakati wa kupunguza nguvu za upinzani na kugawanya kura za eneo la Mlima Kenya?
Maswali hayo yamezua mijadala mikali miongoni mwa wachambuzi wa siasa.
Mchambuzi wa masuala ya kisiasa na mhadhiri katika Chuo Kikuu cha Multimedia nchini Kenya, Profesa Gitile Naituli, anaamini hatua hiyo inaweza kumfaidi Rais Ruto kisiasa, hasa katika eneo la Mlima Kenya ambalo limezidi kuonyesha kutoridhishwa na serikali ya Kenya Kwanza.
“Huu ni mpango wa Ruto,” alisema Profesa Naituli.
Kwa mujibu wake, Mlima Kenya ni eneo muhimu kutokana na idadi kubwa ya wapigakura, na njia moja ya kudhoofisha upinzani dhidi ya Rais ni kugawanya viongozi wa kisiasa wa eneo hilo.
“Lengo la Ruto ni Mlima Kenya, ambao una idadi kubwa zaidi ya wapigakura. Njia pekee ya kushinda bila uungwaji mkono wa eneo hilo ni kuligawanya kisiasa,” alisema.
Hata hivyo, wafuasi wa Nyoro pamoja na baadhi ya wachambuzi wamekataa mtazamo huo wakisema viongozi wengi kutoka Mlima Kenya tayari wameonyesha nia ya kuwania urais bila kusawiriwa kuwa wanatekeleza ajenda ya Rais.
Kwa sasa eneo hilo lina wanasiasa kadhaa wenye matarajio ya urais wakiwemo kiongozi wa DCP Rigathi Gachagua, Martha Karua wa PLP, Jimmy Wanjigi wa Safina, Justin Muturi wa Democratic Party na Peter Munya wa PNU.
Mchambuzi mwingine wa kisiasa, Dismas Mokua, anasema si sahihi kukichukulia chama cha Nyoro kama mradi wa Ikulu.
“Kenya ni nchi ya kidemokrasia na kila raia ana haki ya kuanzisha chama, kuwania katika uchaguzi na kufuatilia ndoto zake za kisiasa,” alisema Mokua.
Aliongeza kuwa hata kama Nyoro angekuwa anatekeleza ajenda ya mtu mwingine, Katiba bado inamruhusu kuongoza chama cha kisiasa na kuwania nafasi yoyote ya uongozi.
Mokua alisema kuwabeza viongozi wanaoanzisha vyama vipya bila ushahidi ni aina ya siasa za upotoshaji.
Aidha, alionya kuwa Wakenya hawapaswi kushangaa iwapo Rais Ruto atatumia mbinu mbalimbali za kisiasa kujinufaisha kabla ya uchaguzi wa 2027.
“Hakuna viwango vya ubora katika siasa. Wagombeaji wa urais hutumia mbinu zote zinazoweza kuwasaidia kushinda uchaguzi,” alisema.
Lakini Profesa Naituli anahisi Nyoro yuko katika hatari ya kuonekana kama sehemu ya mfumo wa utawala badala ya mwanasiasa huru.
“Alikuwa kiongozi mchanga aliyekuwa akiibuka, lakini sasa ameanza kuvunja matumaini ya watu,” alisema.
Kwa upande wake, Nyoro amesisitiza kuwa uamuzi wake hauna uhusiano na makubaliano yoyote ya siri na Ikulu bali umetokana na maslahi ya taifa.
Akizungumza wakati wa uzinduzi wa PPK, alisema amekuwa akifanya mashauriano kwa miezi mingi na viongozi wa vyama mbalimbali kabla ya kuondoka UDA.
“Moyo wangu umelemewa kwa miezi mingi. Nimekuwa nikiomba kwamba uamuzi wowote wa kisiasa nitakaochukua uwe na maslahi ya Wakenya mbele,” alisema.
Alisisitiza kuwa alijitenga na serikali na chama tawala muda mrefu uliopita.
“Ni wazi tuliondoka serikalini zamani. Kwa kumbukumbu sahihi, tulijitenga na UDA na serikali ya wilibaro kitambo sana. Kuanzia leo, Peoples’ Party of Kenya iko rasmi katika upinzani,” alisema.
Hatua hiyo ni mabadiliko makubwa kwa mwanasiasa ambaye hapo awali alikuwa miongoni mwa vijana waliotambulika zaidi ndani ya serikali ya Kenya Kwanza.
Umaarufu wake uliongezeka kwa kasi kiasi cha kuwafanya wengi kumchukulia kama mmoja wa viongozi ambao wangemrithi Rais Ruto siku zijazo.
Ingawa hakutangaza waziwazi kwamba atawania urais mwaka 2027, kauli zake zilionyesha kuwa anajitayarisha kwa wadhifa mkubwa zaidi nchini.
Alifichua kuwa amefanya mashauriano ya kina na viongozi wa upinzani wakiwemo Rigathi Gachagua, Kalonzo Musyoka, Martha Karua, Peter Munya, James Orengo na Dkt Fred Matiang’i.
Changamoto kubwa sasa kwa Nyoro, kwa mujibu wa wachambuzi, ni kuwashawishi Wakenya kuwa kuvunja kwake uhusiano na UDA ni jambo la kweli na si mbinu nyingine ya kisiasa.