ODM yafichulia Jopo la Mizozo ya Vyama sababu za kumfurusha Sifuna
CHAMA cha Orange Democratic Movement (ODM) kimefafanua rasmi sababu za kumwondoa Seneta wa Nairobi, Edwin Sifuna, katika wadhifa wa Katibu Mkuu, kikitaja kile kilichoeleza kama miezi kadhaa ya kutoelewana, kukosa kuhudhuria mikutano muhimu, kuanzisha mikakati ya kisiasa sambamba na misimamo ya chama pamoja na matamshi ya umma yaliyodaiwa kusababisha mkanganyiko ndani ya chama.
Katika stakabadhi zilizowasilishwa mbele ya Jopo la Kutatua Mizozo ya Vyama vya Kisiasa (PPDT) jijini Nairobi, ODM inasema mzozo huo si njama ya kisiasa ya kumtimua kiongozi, bali ni mchakato wa kinidhamu ulioanzishwa baada ya juhudi za upatanishi kushindikana na madai ya ukiukaji wa mara kwa mara wa maamuzi ya vikao vya chama.
Chama kinataka kesi ya Bw Sifuna itupiliwe mbali kwa hoja kuwa hakufuata kwanza mifumo ya ndani ya kutatua migogoro kabla ya kukimbia mahakamani.
Katika hati ya kiapo ya Halima Daro, mwanachama wa Kamati Kuu ya Kitaifa (NEC) na katibu wa makundi maalum, chama kinadai mahakama hiyo haina mamlaka ya kusikiliza kesi hiyo kwa kuwa taratibu za ndani hazijatumika kikamilifu.
Bi Daro alisema mchakato wa kumwondoa Sifuna ulitokana na “makosa mbalimbali, ikiwa ni pamoja na kuwa na msimamo tofauti na wa chama katika masuala nyeti na hivyo kuhatarisha uadilifu wa chama na kamati zake.”
Kwa mujibu wa stakabadhi za mahakama, mivutano ilianza Julai 2025 wakati Kamati Kuu ya ODM ilipokutana Karen baada ya Sifuna kuonekana katika kipindi cha The Explainer cha runinga ya Citizen.
Katika mahojiano hayo, alidai kuwa mkataba wa maelewano kati ya ODM na chama cha United Democratic Alliance (UDA) ulikuwa “umekufa.”
Kauli hiyo ilisemekana kukinzana na maazimio ya awali ya chama ambayo marehemu kiongozi wa ODM Raila Odinga, alisisitiza umuhimu wa Katibu Mkuu kuzingatia na kutetea misimamo rasmi ya chama katika matamshi yake ya umma.
Inadaiwa kuwa hata baada ya kusoma maazimio ya kikao hicho mbele ya wanahabari, Sifuna aliendelea kutoa kauli zinazodaiwa kukinzana na misimamo ya chama, hata baada ya kifo cha Odinga Oktoba 2025.