Omanga afunguka sababu za kumtema Ruto
ALIYEKUWA Seneta Maalum Millicent Omanga hatimaye amevunja kimya chake kuhusu mabadiliko yake ya kisiasa, akieleza kuwa alijitenga na Rais William Ruto kutokana na kile anachodai kuwa ni usaliti wa ahadi na kuyumba kwa misingi ya uongozi serikalini.
Omanga, ambaye alikuwa sura maarufu katika kampeni za Kenya Kwanza katika uchaguzi mkuu wa 2022, anasema alitengana na Rais miaka mitatu iliyopita baada ya kugundua kuwa ahadi nyingi zilizotolewa kwa Wakenya hazikutekelezwa.
Katika mahojiano maalum, alisema kuwa mara tu baada ya uchaguzi, Rais Ruto alibadili mkondo na kuanza kupuuza ahadi muhimu, hasa zile zilizolenga wanawake na wananchi wa kipato cha chini.
Alisema kuwa badala ya kupunguza mzigo wa maisha, serikali iliongeza ushuru uliowaumiza zaidi wananchi wa tabaka la chini.
“Wananchi wa kawaida wamelemewa na ushuru unaowanyang’anya kipato chao,” alisema.
Miongoni mwa ahadi alizotaja ni mkataba wa wanawake uliotiwa saini hadharani kabla ya uchaguzi, ukiahidi usawa wa kijinsia wa asilimia 50 serikalini.
Pia, kulikuwa na ahadi ya kutoa sodo bure kwa wanafunzi wa shule za umma na msaada kwa kina mama wanaojifungua katika hospitali za umma. Hata hivyo, Omanga anasema hakuna hata moja iliyotekelezwa.
“Kutiwa saini kulikuwa hadharani, lakini baada ya uchaguzi kila kitu kilisahaulika. Hata mpango wa Linda Mama uliondolewa ilhali ulikuwa unasaidia kina mama kujifungua bure,” alisema.
Kwa mtazamo wake, serikali imewatumia wanawake kisiasa kisha ikawaacha. “Wanawake hutumika kwa kura zao lakini hawapewi nafasi katika uongozi,” aliongeza.
Omanga pia alitetea uamuzi wake wa kuhama kutoka chama cha United Democratic Alliance (UDA) na kujiunga na Democracy for Citizens Party (DCP), akisema uamuzi huo ulitokana na misingi yake ya kisiasa.
“Mimi ni mmoja wa waanzilishi wa UDA na nimefanya kazi na Rais kwa muda mrefu tangu nyakati za URP hadi Jubilee. Huu si uamuzi wa hofu bali ni wa kanuni,” alisema.
Katika hatua iliyoonyesha msimamo wake, Omanga alikataa uteuzi katika Tume ya Urejeshaji wa Mito ya Nairobi akisema usingekuwa wa haki kwa wapiga kura wake wengi wanaoishi karibu na mito hiyo.
“Siwezi kushiriki katika mpango utakaowafurusha watu walionichagua,” alisema.
Akipima utendaji wa serikali, aliipa alama ya chini akisema maisha ya Wakenya yamezidi kuwa magumu tangu 2022.
Alisema watumishi wa umma wanakabiliwa na makato mengi bila nyongeza ya mishahara, hali inayowaathiri wao na familia zao.
Alikosoa pia ushuru wa nyumba akisema unazua maswali mengi kuhusu nani anafaidika.
“Ikiwa Wakenya wanachangia na serikali inatoa ardhi, kwa nini wale wanunue nyumba hizo?” alihoji.
Omanga alikiri kuwa kuongoza si kazi rahisi, akisema hata yeye alidhani ni rahisi kabla ya kuwa karibu na serikali. Hata hivyo, alionya kuwa kukosa maandalizi si kisingizio cha kushindwa kutekeleza ahadi.
Alikosoa pia mtindo wa uongozi wa Rais, hasa matamshi ya hadharani yanayodhalilisha watu binafsi.
“Urais unapaswa kuwa ishara ya umoja, si jukwaa la matusi,” alisema.
Alitoa wito kwa viongozi wa upinzani kuungana kuelekea uchaguzi ujao ili kutoa uongozi mbadala na thabiti.
Kuhusu siasa za Nairobi, Omanga alisema atazingatia kuwawezesha wanawake na vijana, kupambana na ukatili wa kijinsia na kuboresha uwajibikaji katika uongozi. Aidha, alisisitiza umuhimu wa kujumuisha mtoto wa kiume katika ajenda za maendeleo ili kuepuka pengo la kijinsia siku zijazo.