Polisi kwa mara nyingine waendeleza ukatili dhidi ya waandamanaji
SAWA na ilivyoshuhudiwa mwaka jana, polisi waliotumwa kudhibiti maandamano ya Jumanne walitumia nguvu kupita kiasi, wakirusha vitoa machozi kwa fujo, kutumia magari ya kurusha maji ya mwasho na hata kufyatulia waandamanaji risasi.
Kufikia jioni jana, watu sita walikuwa wamepoteza maisha mmoja kwa kupigwa risasi.
Kwa mujibu wa wachambuzi wa masuala ya usalama waliozungumza na Taifa Leo, mbinu za maafisa wa usalama zilichochea zaidi hasira miongoni mwa waandamanaji na kuwapa nguvu katika nia yao ya ‘kuonyesha serikali kwamba hawawezi kupuuzwa.’
Wataalamu hao wanasema serikali ilifanya makosa makubwa kwa kushindwa kukusanya habari za kijasusi, kukosekana kwa utaratibu na ukosefu wa mikakati madhubuti ya kushughulikia hali ya dharura.
Hali kama hiyo ilishuhudiwa mwaka jana wakati maandamano yaliyomalizika kwa waandamanaji kuvamia Bunge.
Mtaalamu wa usalama, Bw George Musamali, alitaja kushindwa kwa serikali kutambua ukubwa wa maandamano hayo kuwa “kuporomoka kabisa kwa mfumo wa usalama wa kitaifa na ujasusi.”
“Ni aibu kwa mfumo wetu wa ujasusi. Gen Z walitumia mitandao kupanga maandamano kote nchini. Haya ni maeneo ya kidijitali ambayo maafisa wetu wa kijasusi bado hawajayamilisi. Serikali ilipogundua kilichokuwa kikiendelea, tayari hali ilikuwa imeharibika,” alisema.
Bw Musamali alisema kuwa vuguvugu hilo la kidijitali lisilo na kiongozi, lisilo na ofisi na lililochipuka na kuendeshwa mtandaoni pekee, lilifanya vigumu kwa serikali kutumia mbinu za kawaida za kudhibiti maasi ya raia.
“Hakukuwa na mtu wa kukamata, ofisi ya kuvamia wala kundi la kupigwa marufuku. Ndio maana ilishindwa kabisa. Serikali ilijaribu kupambana na nguvu za kidijitali kwa kutumia mbinu za kizamani,” alieleza.
Matumizi ya nguvu na risasi yaliwafanya waandamanaji kuungana zaidi, wakielekea kwa pamoja kuwavamia polisi,
Mwenyekiti wa Chama cha Kampuni za Kibinafsi za Ulinzi (PSIA), Bw Cosmas Mutava, alikubaliana na Bw Musamali, akisema kilichoshangaza zaidi maafisa wa usalama ni jinsi vijana walivyoweza kujipanga kwa kutumia teknolojia bila kujulikana.
“Inahitaji mtazamo mpya kabisa wa jinsi tunavyojiandaa na matukio ya namna hii. Lazima tujiandae kimtandao,” alisema Bw Mutava.
Baada ya maandamano ya mwaka jana, serikali ilizindua msako mkali dhidi ya wakosoaji.
“Huwezi kupambana na waandamanaji wasio na silaha kwa risasi. Matumizi ya risasi ni kinyume cha sheria na hayakuhitajika. Yalizidisha mzozo badala ya kuutuliza,” alisema Bw Musamali.
Bw Mutava aliongeza kuwa matumizi ya risasi dhidi ya raia ni uvunjaji wa haki za binadamu na sheria.
Alisema kuwa polisi wangetumia mbinu zisizo hatari kama vile mawasiliano bora na njia za kudhibiti umati bila vurugu.
Mashirika ya kutetea haki yameripoti visa vya watu kupotezwa kwa nguvu, kukamatwa kiholela na kuteswa. Waathiriwa hunyimwa haki ya mawasiliano na familia au mawakili.
“Maafisa wa usalama hawawezi kuendesha operesheni kama wanamgambo. Kila kukamata mtu lazima kuwe halali. Vinginevyo tunakiuka Katiba,” alionya.