Habari za Kitaifa

Polisi wachunguza kifo cha Mchina katika uwanja unaojengwa wa Talanta Stadium

Na HILLARY KIMUYU April 3rd, 2026 Kusoma ni dakika: 1

UCHUNGUZI umeanzishwa kubaini kilichosababisha kifo cha mfanyakazi raia wa China katika eneo kunakojengwa uwanja wa Talanta Sports City, Jamhuri, Nairobi.

Kwa mujibu wa maafisa wa usalama, mwili wa marehemu ulipatikana ndani ya choo katika eneo la ujenzi.

Inadaiwa kuwa mpishi anayefanya kazi na timu ya wasimamizi wa ujenzi wa uwanja huo ndiye aliyegundua mwili huo mapema Jumanne asubuhi.

Wafanyakazi wengine pamoja na maafisa wa usalama walifika eneo la tukio haraka kabla ya mwili huo kupelekwa katika hospitali ya karibu, ambako madaktari walithibitisha alikuwa amefariki.

Polisi walifanya uchunguzi wa awali katika eneo hilo na kubaini kuwa marehemu alikuwa na jeraha dogo upande wa kulia wa kichwa.

Mwili huo ulihamishiwa katika Mochari ya Lee kwa uchunguzi wa maiti ili kubaini chanzo halisi cha kifo.

Kamanda wa Polisi eneo la Nairobi Issa Mohamud, alisema kuwa maafisa wa upelelezi wanachunguza iwapo kifo hicho kilitokana na sababu za kawaida au iwapo kuna njama nyingine.

Tukio hilo linajiri miezi michache baada ya mfanyakazi mwingine, Sammy Kyengo mwenye umri wa miaka 35, kupatikana amefariki katika eneo hilo hilo la ujenzi.

Kyengo alikuwa ameripotiwa kupotea na mkewe baada ya kukosa kurejea nyumbani.

Baada ya msako wa wiki moja, mwili wake ulipatikana ndani ya tangi la maji lililokuwa limefichwa chini ya jukwaa la uwanja.

Uchunguzi wa maiti ulionyesha kuwa alikuwa na majeraha kichwani na mgongoni, huku damu ikitoka puani na mdomoni.

Mkewe alisema marehemu alikuwa akilalamikia kucheleweshwa kwa mishahara na alinuia kuacha kazi baada ya kulipwa.

Tukio hilo lilisababisha kusimamishwa kwa muda kwa shughuli za ujenzi huku uchunguzi ukiendelea.

Uwanja huo wa kisasa wenye nafasi ya watu 60,000 unatarajiwa kuwa miongoni mwa viwanja vitakavyotumika katika mashindano ya AFCON 2027.