Habari za Kitaifa

Polisi waliua watu 65 katika maandamano Juni, Julai na kuficha ukweli, IPOA yafichua

Na STEVE OTIENO July 25th, 2025 Kusoma ni dakika: 2

WATU 65 walipoteza maisha, 41 kati yao kwa kupigwa risasi na maafisa wa polisi, huku raia 342 wakijeruhiwa vibaya wakati wa maandamano ya Juni 25 na Julai 7, inasema ripoti mpya ya Mamlaka Huru ya Kuchunguza Utendakazi wa Polisi (IPOA).

Kwa jumla, watu zaidi ya 90 walipigwa risasi baadhi kwenye kifua, tumbo, hata kichwani. Licha ya idadi kubwa ya vifo, IPOA imelaumu Huduma ya Kitaifa ya Polisi kwa kuripoti vifo vitano pekee kati ya 65.

IPOA ilisema kutotoa ripoti kamili kwa makusudi ni ukiukaji wa wajibu wa uwajibikaji, na kunadhihirisha hulka ya taasisi kuficha ukweli.

Ili kuthibitisha chanzo cha vifo hivyo, IPOA ililazimika kushiriki upasuaji wa miili 61 ikijitegemea.

Mamlaka hiyo ilionya kuwa kuficha taarifa kunahujumu haki na kunaleta dhana kwamba polisi wa Kenya wako juu ya sheria.

Haya ni miongoni mwa matokeo yaliyotajwa katika ripoti ya Julai 2025 ya IPOA iliyopewa jina “Ripoti ya kufuatilia Majibu ya Polisi kwa Maandamano ya Umma kati ya Juni na Julai 2025”.

Ripoti hiyo haiishii kuhesabu walioumia pekee, bali inafichua mapungufu ya kimuundo ya jinsi serikali ilivyoshughulikia maandamano, ikianika mfumo wa polisi ulio katika hali ya mgogoro mkubwa.

Kosa kuu lililobainika ni matumizi ya nguvu kupita kiasi. Licha ya Ibara ya 37 ya Katiba ya Kenya kuhalalisha maandamano ya amani, polisi walihusisha maandamano hayo na vurugu na kuyakabili kama machafuko.

Kutoka mwanzo, maafisa walitumia vitoa machozi, magari ya maji ya kuwasha, risasi za mpira, na hata risasi halisi dhidi ya waandamanaji ambao wengi hawakuwa na silaha.

“Majibu ya polisi yalikuwa ya kikatili, mara nyingi ya kifo,” ilisema ripoti hiyo.

Hata baada ya amri ya mahakama kutaka polisi wavalie sare rasmi na vitambulisho vinavyoonekana, maafisa wengi walionekana wakifanya kazi bila nambari za kuwatambua, wakiwa wameficha uso.

Magari ya polisi pia hayakuwa na alama yoyote ya kuyatambua, hali iliyofanya wasiweze kuwajibishwa.

Hali hiyo ilikiuka moja kwa moja Sheria ya Polisi (CAP 84), na kuwaacha waathiriwa wa ukatili wa polisi bila njia ya kuwatambua au kuwafungulia mashtaka waliowadhuru.