Habari za Kitaifa

Presha Naibu Mkuu wa Polisi Eliud Lagat aende wadogo zake wachunguze kesi

June 12th, 2025 Kusoma ni dakika: 3

HUKU shinikizo za kumtaka Naibu Inspekta Jenerali wa Polisi Eliud Lagat ajiuzulu kuhusiana na mauaji ya mwanablogu Albert Ojwang’, Rais William Ruto amewataka Wakenya kudumisha utulivu kuruhusu uchunguzi kuhusu kifo hicho ukamilishwe.

Huku akiungama kuwa kisa hicho kimeibua kero kubwa miongoni mwa Wakenya wa matabaka yote, Dkt Ruto aliwaonya Wakenya dhidi ya kufikia maamuzi fulani aliyodai yanaweza kuingilia uchunguzi unaoendeshwa na Mamlaka ya Kuchunguza Utendakazi wa Polisi (IPOA).

“Tunapoomboleza kifo cha kijana huyu, tuwe watulivu na tufuatilie kwa makini uchunguzi unaoendelea bila kufanya maamuzi ya mapema au kulaumu watu fulani kwani tukifanya hivyo tutavuruga shughuli hiyo na hata matokeo yake,” Rais Ruto akasema jana kwenye taarifa huku akitoa risala za rambirambi kwa familia ya Ojwang’.

Na mapema jana asubuhi, Bunge la Seneti lilisitisha shughuli zake za kawaida na kutenga muda kusikiza maelezo kuhusu suala hilo, kutoka kwa Waziri wa Usalama Kipchumba Murkomen, Inspekta Jenerali wa Polisi Douglas Kanja huku maseneta wakishinikiza kujiuzulu kwa Lagat.

Wengine walioandamana na wawili hao ni Mkurugenzi wa Idara ya Upelelezi wa Jinai (DCI) Mohamed Amin, Naibu Mwenyekiti wa IPOA Bi Anne Wanjiku na Naibu Mwenyekiti wa Tume ya Kitaifa ya Huduma kwa Polisi (NPSC) Edwin Kiprono Cheluget.

Lakini hata kabla ya wakuu hawa wa vitengo hivyo vya usalama kuwasilisha taarifa zao, maseneta, wakiongozwa na kiongozi wa wengi Aaron Cheruiyot walimtaka Bw Lagat ajiuzulu kwa kuhusishwa na kukamatwa kwa Ojwang.’

“Lagat ni rafiki yangu. Lakini kwa sababu ndiye alikuwa mlalamishi katika kesi ya Ojwang’ ambaye sasa ni marehemu baada ya kuuawa katika seli ya polisi, anapasa kukaa kando hadi uchunguzi utakapokamilika,” akasema.

“Ilivyo sasa rafiki yangu Lagat, hamna Mkenya yeyote atakayeamini kuwa hahuhusiki na kifo cha Ojwang,’” akaongeza Seneta huyo wa Kericho, ambaye ni mshirika wa karibu wa Rais Ruto.

Naibu Kiongozi wa Wachache Enoch Wambua alimshauri Bw Lagat kwamba, hata baada ya kukaa kando kutoa nafasi ya uchunguzi, bado ataweza kurejea kazini endapo hatapatikana na makosa.

“Naibu Inspekta Jenerali wa Polisi Eliud Lagat alipiga ripoti kwamba, Ojwang’ alimdhalilisha na kumharibia jina kupitia jumbe zilizomhusisha na visa vya utovu wa maadili. Alifanya vizuri kupiga ripoti kwa nia njema. Lakini yaliyofuatia baada ya hapo yameishia na kuuawa kwa Ojwang’ mikononi mwa wadogo wake ndani ya seli ya kituo cha polisi cha Central. Kwa hivyo, sharti ajiondoe kutoa nafasi kwa uchunguzi ili jina lake litakaswe,” akasema seneta huyo wa Kitui.

Maseneta wengine waliomtaka Bw Lagat ajiuzulu ni Moses Kajwang (Homa Bay), Joe Nyutu (Murang’a), Danson Mungatana (Tana River), John Methu (Nyandarua) miongoni mwa wengine.

“Je, ni sharti Eliud Lagat asalie afisini kama Naibu Inspekta Jenerali wa Polisi? Je, Lagat asipokuwa afisini, Shirika la Huduma kwa Polisi litaporomoka?” Bw Nyutu akauliza.

Alipokuwa akitoa maelezo yake kwa maseneta, Inspekta Jenerali Bw Kanja alitoa msururu wa matukio tangu Jumamosi marehemu Ojwang’ alipokamatwa nyumbani kwao Homa Bay hadi akasafirishwa hadi Nairobi.

“Maafisa wanne wa kitengo cha kupambana na uhalifu wa kimtandao katika makao makuu ya DCI, Ijumaa Juni 6, 2025 walisafiri kutoka Nairobi hadi Homa Bay, baada ya kupata kibali cha kukamatwa kwa mshukiwa. Alipelekwa katika kituo cha polisi cha Mawego kabla ya kusafirishwa hadi Nairobi na kuzuiliwa katika kituo cha Central akiwa salama kiakili na kimwili,” Bw Kanja akaeleza.

Hata hivyo, Inspekta Jenerali huyo alidinda kueleza ni kwa nini aliwasimamisha kazi maafisa watano wa kituo cha Central, kuhusiana na kifo cha Ojwang’ na akamsaza naibu wake Bw Lagat.

“Sina mamlaka ya kisheria kujibu swali hilo,” Bw Kanja akasema akijibu swali kutoka kwa Seneta Kajwang’.

Hata hivyo, kulingana na sheria ya NPSC, ni Rais aliye na mamlaka ya kumsimamisha kazi Naibu Inspekta Jenerali wa Polisi.

Wakati huo huo, viongozi wa upinzani wamempa Bw Lagat makataa ya saa 24 ajiuzulu kutokana na kifo cha Ojwang’.

Kwenye kikao na wanahabari jijini Nairobi jana, kiongozi wa Wiper, Kalonzo Musyoka, kiongozi wa chama cha DCP Rigathi Gachagua, Eugene Wamalwa (DAP-Kenya), Justin Muturi (DP), pia waliitaka serikali kutoa ulinzi kwa familia ya Ojwang’.

“Bw Lagat ni mtu ambaye hapasi kuendelea kushikilia wadhifa huo wakati huu uchunguzi bado unaendelea. Kwa hivyo, tunamtaka ajiuzulu haraka ndani ya saa 24 zijazo kwani anaweza kuingilia uchunguzi unaoendelea,” wanasiasa hao wakasema kwenye taarifa iliyosomwa na Bw Muturi.

Presha dhidi ya Bw Lagat pia imetoka kwa wanaharakati wa kutetea haki za kibinadamu ambao wamewasilisha mashtaka ya kibinafsi dhidi ya Bw Lagat.

Wanaharakati hao, Julius Ogogoh, Khelef Khalifa, Francis Auma na Peter Agoro, pia wanataka Mahakama Kuu ya Milimani kutoa agizo la kumzuia Bw Lagat kuingia afisini mwake au kutoa maelezo yoyote wakati uchunguzi unaendelea “hadi atakapokamatwa na kushtakiwa rasmi kortini”.