Habari za Kitaifa

Rais wa Slovenia Nataša Musar ahimiza Wakenya kulinda uhuru wao

Na CHARLES WASONGA June 2nd, 2025 Kusoma ni dakika: 1

RAIS wa Slovenia Nataša Pirc Musar amewahimiza Wakenya kuendelea kulinda matunda ya uhuru wa taifa hili na wakatae kuingiliwa na watawala wanaoendeleza ukoloni mamboleo.

Huku akirejelea kumbukumbu za uongozi wa Rais wa kwanza wa Kenya Hayati Mzee Jomo Kenyatta, kiongozi huyo alielezea kuwa kando na kupigania uhuru wa taifa hili Kenyatta pia alitetea umoja wa Afrika.

“Ndoto hii bado inafaa kuendelezwa kama mwanzoni, kupitia viongozi wa sasa,” akasema alipohutubu Jumapili katika shereha za Madaraka Dei katika Kaunti ya Homa Bay.

Rais Musar alikuwa mgeni wa heshima katika makala hayo ya 62 ya sherehe hizo zilizoandaliwa katika uwanja wa michezo wa Raila Odinga na kuongozwa na Rais William Ruto.

Kiongozi huyo wa taifa la Slovenia alielezea kufurahishwa kwake kuundwa kwa Mkataba wa Biashara huru Barani Afrika (AfCFTA) kuimarisha biashara miongoni mwa mataifa 55 ya bara hilo.

“Nahimiza Kenya kuunga mkono mkataba kama huu wa kibiashara kwani Utaleta manufaa makubwa kwa raia wake, badala ya kutegemea misaada kutoka mataifa ya ng’ambo,” Bi Musar akaeleza huku akielezea kufurahishwa kwake na mapokezi mazuru aliyopewa na mwenyeji wake Rais William Ruto na Wakenya kwa ujumla.

Mkataba wa kibiashara wa AfCFTA ulianzishwa mnamo 2018 na Umoja wa Afrika (AU) kwa ajili ya kubuni soko moja kwa bidhaa kutoka mataifa 55 ya bara hilo.

AfCFTA inalenga kuendeleza biashara baina ya mataifa ya Afrika, kuchochea uzalishaji wa bidhaa na kuimarisha ushirikiano wa kiuchumi na kibiashara baini ya mataifa ya Afrika.