Habari za Kitaifa

Ripoti ya kutisha kuhusu jinsi moto uliua watoto shuleni Hillside Endarasha

Na GITONGA MARETE February 6th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

HUZUNI ilitanda katika mahakama ya Nyeri mnamo Alhamisi wakati simulizi ya kutisha ilipotolewa kuhusu jinsi wavulana 21 walivyopoteza maisha yao, bweni la Shule ya Hillside Academy lilipoteketea mnamo Septemba 5, 2024.

Wazazi wa waathiriwa walijawa na huzuni walipoelezwa kuhusu ripoti zilizoonyesha kuwa watoto wao walipata majeraha ya moto yaliyozidi asilimia 100 huku wakivuta gesi ya sumu ya kaboni, hali iliyosababisha vifo vyao.

Dkt Grace Atieno, daktari aliyeshiriki katika upasuaji wa maiti, aliwasilisha ripoti ya kutisha iliyoeleza kwa kina jinsi kila mmoja wa wavulana hao 21 alivyofariki.

“Sababu kuu ya vifo ilikuwa majeraha makubwa ya moto mwilini kwa asilimia 100 na asilimia 10 ya kuvuta moshi. Sampuli pia zilichukuliwa kwa uchunguzi wa sumu na DNA,” alisema Dkt Atieno.

Alikuwa akitoa ushahidi mbele ya Hakimu Mkazi Mwandamizi Mary Gituma, huku wazazi wa wavulana hao 21 wakitarajia kupata majibu kuhusu mkasa uliowapokonya wapendwa wao.

Baada ya mkasa huo, wazazi walisema waliwekwa gizani kuhusu chanzo cha moto huo bila maelezo yoyote kutoka kwa timu za uchunguzi, na wakataka kufanyika kwa uchunguzi wa kina.

Shahidi wa pili, Bw Dennis Owino, mtaalam katika Maabara ya Serikali, alieleza kuwa baada ya mkasa huo, sampuli za mabaki zilichukuliwa kutoka sehemu mbalimbali za bweni lililoungua na kupelekwa kwa uchunguzi ili kubaini kama kulikuwa na mabaki ya petroli au mafuta ya taa.

Alisema uchunguzi huo ulithibitisha kuwa “hakukuwa na vichocheo vya moto vya kemikali vinavyotokana na mafuta ya petroli vilivyogunduliwa kwenye sampuli zilizowasilishwa.”