Habari za Kitaifa

Ruto alivyopalilia umasikini kwa kufyeka mishahara kupitia ushuru mpya

Na CONSTANT MUNDA June 11th, 2025 Kusoma ni dakika: 3

MNAMO Desemba mwaka jana, Gerald Mbalu alipokea ujumbe mfupi kutoka kwa chama chake cha ushirika na mikopo (SACCO) ukimjulisha kuwa Sh35,220.22 zimewekwa kwenye akaunti yake ya mshahara.

Hata hivyo, aliweza kutoa tu Sh2,681.39 kama salio. Pesa za mshahara wake alizoenda nazo nyumbani zilikuwa asilimia 4.13 pekee ya mshahara wake wa Sh64,950.

Hali hii inakiuka Sheria ya Ajira ya mwaka 2007, ambayo inazuia waajiri kukata zaidi ya theluthi mbili ya mshahara wa msingi wa mfanyakazi ili kulinda haki zao za kiuchumi.

Kwa maelezo zaidi, Bw Mbalu ana mikopo miwili kutoka kwa Sacco hiyo inayoshughulikia mshahara wake: mkopo wa maendeleo na mkopo wa Fosa.

Mkopo wa maendeleo, aliouchukua kwa kutumia hati ya kumiliki ardhi, unakatwa moja kwa moja kwenye mshahara wake, ilhali mkopo wa Fosa unakatwa kwenye akaunti ya mshahara lakini hauonekani kwenye hati ya mshahara.

Aidha, alichukua mkopo wa simu wa Sh60,000 kutoka Sacco hiyo hiyo, unaopaswa kulipwa kwa miezi mitatu, ulioanza kulipwa Desemba.

Malipo ya mkopo huo pia yanakatwa kutoka akaunti yake ya mshahara (Fosa) lakini hayajaorodheshwa kwenye taarifa ya mshahara.

“Ninaenda kazini kila mwezi kulipa mikopo. Kinachobaki kwenye mshahara wangu hutumika kulipia maji na umeme. Mikopo niliyochukua niliweka kwenye biashara inayotusaidia kukimu mahitaji ya msingi, lakini kwa miaka michache iliyopita, mauzo hayajakuwa mazuri kiasi cha kurejesha mikopo hiyo,” anasema Bw Mbalu.

“Nikifutwa kazi leo, nitarudi nyumbani mikono mitupu isipokuwa kwa akiba ya pensheni ya NSSF.”

Kisa cha Bw Mbalu kinawakilisha hali inayowakumba wafanyakazi wengi walio na mikopo waliyochukua awali, hali ambayo imezidi kuwa mbaya kutokana na ongezeko la makato ya lazima kusaidia mpango wa Rais William Ruto wa afya kwa wote na makazi nafuu.

Waajiri wameonya kuwa, kipato halisi cha wafanyakazi kimekuwa kikishuka tangu 2023, jambo linalowasababishia changamoto kubwa za kutimiza sheria za kampuni na taasisi za kifedha.

Shirikisho la Waajiri Nchini (FKE) linakadiria kuwa, makato kwenye mishahara ya wafanyakazi sasa yanachukua kati ya asilimia 40 hadi 45 ya mshahara wa jumla, hali inayopunguza uwezo wa kununua bidhaa katika mazingira ya kiuchumi unaoendeshwa zaidi na matumizi.

“Ikiwa tutaendelea kupunguza malipo ya nyumbani kwa wafanyakazi, watakuwa wakikopa zaidi na kuingia katika hali ngumu ya kifedha, jambo litakalosababisha mzozo wa kijamii,” alionya Mkurugenzi Mkuu wa FKE, Bi Jacqueline Mugo mnamo Januari.

“Watu wataanza kujiuliza faida ya kuwa na ajira ni ipi. Hali hiyo itafanya ajira kuwa haina maana, na tutakuwa na kundi la ‘masikini wanaofanya kazi’ hali ambayo hatutaki kama taifa.”

Mnamo Oktoba mwaka jana, Wizara ya Afya ilianza kukata asilimia 2.75 ya mshahara wa jumla kwa Hazina ya Bima ya Afya ya Jamii (SHIF), miezi kadhaa tu baada ya kuanza kukata asilimia 1.5 ya ushuru wa nyumba kuanzia Julai 2023.

Kufikia Desemba 27 mwaka jana, makato haya mawili yalitozwa ushuru mara mbili, kwani Mamlaka ya Ushuru Kenya (KRA) ilihesabu ushuru wa PAYE kwa kutumia mshahara wa jumla, kabla ya wafanyakazi kupata afueni kupitia Marekebisho ya Sheria za Ushuru ya 2024.

Kuanzia Februari, michango ya NSSF pia itaongezeka ambapo kiwango cha chini kitaongezeka kutoka Sh420 hadi Sh480, huku kiwango cha juu kwa mfanyakazi kikiongezeka kutoka Sh2,160 hadi Sh3,840.

Ili kupunguza mzigo kwa wafanyakazi, FKE mnamo Mei 1 ilipendekeza kuwa makato ya lazima yawekwe kulingana na mshahara wa msingi badala ya mshahara wa jumla, ushuru wa makazi upunguzwe hadi asilimia 0.5 kutoka 1.5, na kiwango cha msamaha wa ushuru kipandishwe kutoka Sh24,000 hadi Sh36,000.

Pesa zilizokusanywa kutoka ushuru wa nyumba zilifikia Sh54.16 bilioni katika mwaka wa kwanza uliomalizika Juni 2024, na zinatarajiwa kuongezeka hadi Sh65.53 bilioni mwaka unaoishia Juni 2025, na Sh95.84 bilioni kwa mwaka unaoanza Julai.

Kupungua kwa mapato ya wafanyakazi kumepunguza mahitaji ya bidhaa na huduma, hali inayozidi kuwa mbaya kutokana na mzunguko hafifu wa pesa huku serikali ikiwa na deni kubwa kwa wasambazaji bidhaa na huduma.

FKE inasema mahitaji duni ya bidhaa na huduma, uhaba wa fedha, ongezeko la gharama za kuendesha biashara, mazingira yasiyotabirika ya ushuru, mabadiliko ya mara kwa mara ya sheria, soko linalozidi kupungua na kupoteza ushindani vimeathiri vibaya mtiririko wa fedha kwa kampuni.

Hali hiyo imezuia kubuniwa kwa nafasi mpya za kazi, huku baadhi ya kampuni zikilazimika kufurusha wafanyakazi wa kudumu na kuwaajiri vibarua.

Mnamo Novemba mwaka jana, KRA ilisema imegundua mwenendo wa kampuni kupunguza mshahara wa jumla kwa wafanyakazi.

Uchambuzi wa KRA wa takwimu za mishahara katika sekta ya kibinafsi kati ya Juni na Septemba ulionyesha mshahara wa wastani wa kila mwezi ulipungua kwa asilimia 2.89 hadi Sh75,781 kutoka Sh78,034 kwa kipindi kama hicho mnamo 2023 – hali isiyokuwa ya kawaida kwa zaidi ya miaka 30.