Habari za Kitaifa

Ruto alivyovunja agano na kanisa ukuruba ukiyeyuka kama umande asubuhi

Na GEORGE MWENDWA, ELVIS ONDIEKI June 9th, 2025 Kusoma ni dakika: 3

RAIS William Ruto alipoingia mamlakani siku 1,000 zilizopita, alikuwa na uhusiano wa karibu sana na viongozi wa makanisa ya Kenya.

Lakini muda mfupi baadaye, uhusiano huo ulianza kudhoofika.

Waliokuwa wafuasi wake wa dhati — washirika wa maombi wakati wa kampeni na watetezi wake wakubwa madhabahuni — sasa wanajiondoa polepole, wakitaja kutoridhishwa na uongozi wake.

Katikati ya hali ngumu ya kiuchumi, misukosuko ya kisiasa, na hasira za umma, mwelekeo mpya wa kanisa unaashiria kupotea kwa imani si tu ya kiroho, bali pia ya kisiasa kwa rais ambaye waliwahi kumuita “mteule wa Mungu”.

Uhusiano kati ya Kanisa na Serikali ulionekana kuwa wa amani, hadi pale makaburi ya halaiki yalipogunduliwa Shakahola mapema mwaka 2024, na kuhusishwa na dhehebu lililoongozwa na Paul Mackenzie.

Tukio hilo lilifichua ukosefu wa usimamizi wa mashirika ya kidini na kuzua maswali kuhusu uzembe au ushiriki wa serikali.

Kama hatua ya kukabiliana na hali hiyo, Dkt Ruto aliunda jopo kazi, ambalo miongoni mwa majukumu yake lilikuwa kudhibiti ongezeko la mashirika ya kidini yenye misimamo mikali na ya ulaghai, pamoja na kutaka makanisa yaanze kulipa kodi kutokana na mapato yao.

Hatua hiyo ilizua upinzani mkali kutoka kwa viongozi wa makanisa ya Kipentekoste, waliodai kuwa serikali ya Ruto ilikuwa inakiuka uhuru wa kuabudu.

Viongozi wa makanisa walipinga Mswada wa Mashirika ya Kidini, ambao hatimaye ulitupiliwa mbali, wakiwa na kauli kama, “heshimu kanisa, huwezi kutuchunguza ilhali ni sisi tuliokuingiza mamlakani.”

Katikati ya mwaka 2024, maandamano dhidi ya ushuru yaliyoongozwa na vijana wa Kenya yalifichua ufa mkubwa zaidi katika uhusiano wa kanisa na serikali ya Ruto.

Mswada wa Fedha wa 2024, uliokuwa na mapendekezo ya kuongeza ushuru kwa bidhaa muhimu, ulisababisha maandamano makubwa. Majibu ya serikali — yaliyojumuisha madai ya utekaji nyara na ukatili wa polisi — yalilaaniwa vikali.

Mwanzoni, viongozi wengi wa kanisa walikaa kimya au kutoa matamshi ya tahadhari, jambo lililosababisha shutuma za kuwa washirika wa maovu.

Hata hivyo, baada ya shinikizo la umma kuongezeka, taasisi kadhaa za kidini zilianza kulalamikia hali hiyo. Baraza la Kitaifa la Makanisa ya Kenya (NCCK) lilikosoa hatua za serikali, likisisitiza haja ya uwajibikaji na haki.

Viongozi wa Kanisa Katoliki na Kanisa la Anglikana la Kenya pia walilaani ukatili na kuhimiza serikali kuheshimu haki za raia.

Katika hatua ya kipekee, baadhi ya makanisa yalichukua hatua za kusaidia waandamanaji. Kanisa la All Saints’ Cathedral Nairobi lilifungua milango yake kwa waandamanaji waliokuwa wakikimbia polisi, huku CITAM wakipiga marufuku wanasiasa kuzungumza madhabahuni, wakikubaliana na mwito wa vijana wa kutaka ibada na siasa kutenganishwa.

Kwa kuashiria mabadiliko ya wazi, makanisa kadhaa yalianza kukataa michango kutoka kwa wanasiasa, akiwemo Dkt Ruto. Dayosisi ya Nairobi ya Kanisa Katoliki ilikataa mchango wa Sh5 milioni, wakieleza wasiwasi kuhusu uhuru wa kanisa na maadili ya kupokea pesa kutoka kwa serikali inayokosolewa vikali.

Kanisa la Anglikana pia lilikataa mchango wa Sh5 milioni, likionesha mwelekeo mpya wa kutotaka kuingiliwa kisiasa.

Mnamo Mei 14, Askofu Maria Wainaina wa Dayosisi ya Murang’a ya Kanisa Katoliki alikataa zawadi zilizotolewa na w madiwani wa Bunge la Kaunti ya Kirinyaga, badala yake akataka zielekezwe kusaidia shule ya watoto viziwi ya Kerugoya.

Msaada huo ulikuwa ni pamoja na Sh600,000 kwa wanakwaya na Sh2 milioni za kujenga nyumba ya padri.

Sakata la kutimuliwa kwa aliyekuwa Naibu Rais Rigathi Gachagua pia imechangia hali hiyo. Katika ibada ya Kanisa Katoliki huko Embu mnamo Novemba 2024, matusi na kelele kutoka kwa waumini ziliashiria hasira dhidi ya hatua hiyo.

Viongozi wa makanisa waliowahi kuwaunga mkono Dkt Ruto na Bw Gachagua sasa wanajikuta njia panda. Mikutano kadhaa ya kidini iliyohudhuriwa na Bw Gachagua iligeuka vurugu, huku akilaumu serikali ya Ruto kwa “kudharau kanisa”.

Katika mahubiri kadhaa, wachungaji wameonyesha majuto na kuvunjika moyo.

“Nilifikiri serikali hii ni ya Mungu; kumbe ni serikali ya vita,” alisema Teresia Wairimu wa Faith Evangelistic Ministry.

Mchungaji Tony Kiamah wa River of God Church aliifananisha serikali na mwizi, akinukuu injili ya Yohana, na kuangazia gharama ya juu ya maisha, ufisadi, na kukandamiza sauti za upinzani kama ushahidi wa uozo wa maadili serikalini.

“Hii si serikali ya Mungu. Tutawatambua kwa matunda yao, na hapa hakuna tunda la Mungu,” alisema.

Aliendelea: “Viongozi wetu wa makanisa, ni lazima tukubali kuwa tulikosea. Tulichokifanya kilikuwa kosa.”

Bi Wairimu naye alisema kwa masikitiko.

“Katika uchaguzi ujao, ni lazima mnishawishi, wengi wenu mtaenda nyumbani.”

Kihistoria, kanisa la Kenya limekuwa nguzo muhimu katika kutetea haki za kijamii na mageuzi ya kisiasa. Viongozi kama Askofu Henry Okullu, Askofu Alexander Muge, na Askofu Mkuu Ndingi Mwana ‘a Nzeki walikuwa nguzo katika mapambano ya haki za binadamu.

Edwin Kegoli, mchambuzi wa sera na siasa, anaamini uhusiano huo umefika mwisho.

“Katika kampeni ya 2022, Ruto alitumia ucha Mungu wa Wakenya na uhalisia kwamba makanisa hutoa majukwaa tayari. Aliwahadaa Wakenya kwa kutumia imani yao na hisia zao. Alijifanya kuwa mhanga wa dhuluma ya serikali ya awali, na akawavuta waumini upande wake.”

“Lakini baada ya kuchukua mamlaka, watu waliokuwa na matumaini makubwa waliona hali ikizidi kuwa mbaya. Uchumi umezidi kuwa mgumu. Sasa ni kama hakuna kurudi nyuma. Kwa sasa hawezi tena kujiunga na kanisa au kutumia madhabahu kwa ajenda ambazo ni ngumu kuzitekeleza.”

Rev Mutava Musyimi, mmoja wa wachache waliowahi kuwa viongozi wa dini na siasa, alisema ingawa hayuko tayari kutoa maoni ya kina kuhusu uhusiano wa Ruto na Kanisa, si kila mwanasiasa anayekaribia kanisa ni mnafiki.