Ruto, Raila waonya dhidi ya kampeni za mapema kabla ya 2027
RAIS William Ruto na Waziri Mkuu wa zamani Raila Odinga Jumatano walitoa wito wa amani huku maelfu ya vijana wakijaa kwenye miji katika kaunti mbalimbali kwa ukumbusho wa mauaji ya Gen Z ya mwaka jana.
Viongozi hao ambao ukuruba wao ulipatikana baada ya maafa yaliyotokana na maandamano ya kupinga Mswada wa Fedha 2024, walikuwa wanahudhuria hafla ya mazishi ya babake Gavana wa Kilifi Gideon Mung’aro.
Maandamano ya mwaka jana yaliacha zaidi ya watu 60 wakiwa wamekufa na mamia zaidi kupata majeraha.
“Naomba wale walio na mtazamo tofauti na wetu na wanaoshiriki maandamano, msizue ghasia kiasi cha kuharibu mali na kutatiza amani ya nchi yetu; hatuna nchi nyingine ya kwenda,” akasema Rais Ruto.
Maandamano hayo yalifanyika katika zaidi ya kaunti 25.
Sehemu zingine ghasia zilizuka na uporaji mkubwa wa mali kufanyika huku waandamanaji wakikemea ukatili wa polisi na kutaka waliouawa mwaka jana kutendewa haki.
Rais vile vile alishambulia viongozi aliosema tayari wameanza kampeni za mapema za uchaguzi wa 2027.
Kulingana na yeye, nguvu zake zote zipo katika kutekeleza maendeleo na kutimiza ahadi zake za kubadilisha maisha kupitia afya, kilimo, nyumba nafuu na muundomsingi.
“Nataka kumshukuru Bw Odinga kwa kukubali kuunganisha nchi kwa sababu la muhimu zaidi ni taifa letu. Hatuhitaji kujiingiza kwenye siasa za kila siku. Uchaguzi hufanyika siku moja lakini maendeleo ni ajenda ya muda mrefu,” akasema.
Bw Odinga alisihi Wakenya kuacha hulka ya kushiriki siasa kila siku na kampeni za mapema. Hata hivyo, alisisitiza haja ya kuheshimu haki za raia kuandamana kwa amani.
Kinara huyo wa ODM aliponda wanasiasa wa upinzani akiwemo aliyekuwa Naibu Rais Rigathi Gachagua na Kinara wa Wiper Kalonzo Musyoka kwa kuendeleza kampeni za mapema.
“Hatuwezi kufanya kampeni kwa miaka mitano mizima. Tunahitaji amani na pindi uchaguzi unapokwisha, tusubiri hadi muda ufaao kuanza kampeni tena,” akasema Bw Odinga.