Habari za Kitaifa

Samidoh kukamatwa kwa ‘kuhepa’ kazi ya polisi

Na BENSON MATHEKA June 10th, 2025 Kusoma ni dakika: 1

MWANAMUZIKI maarufu wa Mugithi ambaye pia ni afisa wa polisi Samuel Muchoki almaarufu Samidoh, anatafutwa kukamatwa wakati wowote kwa madai ya kutoweka kazini.

Wakubwa wake katika Huduma ya Kitaifa ya Polisi (NPS) wameagiza akamatwe kwa kutoripoti kazini kwa zaidi ya siku 10.

Kulingana nao, Samidoh hajafika kazini tangu Mei 27, 2025, kufuatia kuhamishwa kwake hadi Kitengo cha Kukabiliana na Wizi wa Mifugo (ASTU) huko Gilgil.

Ripoti ya polisi iliyotiwa saini na kamanda wa ASTU na kuonwa na Taifa Leo inasema kuwa Samidoh hakuripoti kazini tangu Mei 27, 2025 baada ya likizo yake rasmi kumalizika.

 “Tafadhali fahamu kuwa Samuel Ndirangu Muchoki afisa nambari ya kazi 247569/2013040010 APC wa Kitengo cha Kukabiliana na Wizi wa Mifugo alipewa likizo na alitakiwa kuripoti kazini tangu 27/05/2025, lakini hakufanya hivyo,” ripoti hiyo imesema kwa sehemu.

“Tangu wakati huo, hajaonekana, na mahali alipo kwa sasa hapajulikani. Juhudi za kumtafuta hazijazaa matunda. Kwa sasa ameacha kazi bila ruhusa kwa kipindi kinachozidi siku 10 na hivyo anatangazwa kuwa mtoro kuanzia Juni 6, 2025.”

Kulingana na Sheria ya Huduma ya Kitaifa ya Polisi, afisa yeyote akikosa kufika kazini bila ruhusa au sababu ya msingi kwa zaidi ya siku kumi huchukuliwa kuwa ameacha kazi.

“Afisa wa polisi ambaye akikosa kufika kazini bila ruhusa au sababu ya msingi kwa kipindi kinachozidi siku kumi, isipothibitishwa vinginevyo, atachukuliwa kuwa ameacha kazi katika Huduma.”

“Afisa yeyote wa polisi ambaye atatoroka kutoka Huduma anafanya kosa na anaweza kufukuzwa kazi moja kwa moja au kuhukumiwa kifungo kisichozidi miaka miwili akipatikana na hatia,” inasema Sheria ya Huduma ya Kitaifa ya Polisi.